Vita nchini Ukraine: Saudi Arabia inataka kuwa mpatanishi kwa kuandaa mazungumzo Jeddah
Saudi Arabia inapanga kufanya mazungumzo tarehe 5 na 6 Agosti kujadili njia za kukuza amani nchini Ukraine, yakihudhuriwa na wawakilishi kutoka Kiev, madola ya Magharibi na nchi zinazoendelea, sawa na nchi 30… lakini bila Urusi. Mzozo umeendelea kushika kasi, na hakuna upande ulioweza kudhibiti eneo lolote muhimu katika miezi ya hivi karibuni.
Imechapishwa:
Tangu Washington ilishutumu Riyadh kwa kuegemea upande wa Urusi katika kuweka bei ya mafuta kuwa juu, Saudi Arabia na Mwanamfalme wake Mohammed bin Salman (MBS) wanataka kuchukua nafasi kubwa katika diplomasia ya kimataifa.
Mwezi Mei, Saudi arabia ilimkaribisha rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky katika mkutano wa kilele wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu, ambapo aliwashutumu baadhi ya viongozi wa Kiarabu kwa kufumbia macho ukatili unaofanywa na Urusi.
Lakini Saudi Arabia pia ilichaguliwa kuwa mwenyeji wa mazungumzo hayo kwa sababu ya uhusiano wake wa karibu na China: Mapema mwaka huu, Beijing ilisaidia kutatua mgogoro kati ya Saudi Arabia na adui yake wa kikanda Iran. Kwa sababu hizi, nchi za Magharibi zinatumai kuona China ikijipatia nafasi wakati wa majadiliano huko Jeddah.
Hasa kwa vile Beijing imerejelea mara kwa mara kwamba inafanyia kazi mpango wa amani wa Ukraine. Hata hivyo, haikushiriki katika mazungumzo ya kwanza yaliyofanyika Copenhagen mwezi uliopita.
Katika mkutano huu wa kilele, maoni ya Ukraine na nchi nyingi zinazoendelea yalitofautiana sana, ambapo Kiev ilitaka kurudishwa kwa maeneo yote yaliyokaliwa na kutaka wanajeshi wa Urusi kuondoka nchini kabla ya kuanza kwa mazungumzo ya amani.