Mafuriko yawaacha watu bila makazi Jonglei
Watu zaidi ya Laki Tano, hawana makazi katika Jimbo la Jonglei nchini Sudan Kusini, kutokana na mafuriko makubwa ambayo yamekuwa yakishuhudiwa kutokana na mvua kubwa ambayo imekuwa ikinyesha kwa karibu miezi mitatu sasa. Mazao pia yameharibiwa kutokana na janga hilo.
Imechapishwa:
Katika taarifa iliyotolewa na Mamlaka ya hali ya hewa nchini Sudan Kusini, iliyoko mji mkuu Juba, mvua isiyo ya kawaida ambayo imekuwa ikinyesha itaendelea kwa muda wa miezi miwili ijayo.
Kuthibitisha kuwa watu wapatao nusu milioni wameachwa mbila makao ni mmoja wa wabunge kutoka jimbo la Jonglei, Deng Dau.
“Mafuriko yamekumba hali ya kila siku ya watu. Watu walioathirika kutokana na mvua na mafuriko wanakadiriwa kuwa nusu milioni. Kila mtu ambaye yuko kwenye jimbo la Jonglei ameathirika. Vijiji vyote vimekumbwa na maji, “ amesema Deng Dau, mmoja wa wabunge wa Jonglei.
“Hali mbaya itatokea hivi karibuni. Ikiwa mashirika ya kimataifa hapa nchini yana misaada ya kuwapa walioathirika, basi yatoe misaada hiyo kwa walengwa, “ amesema kiongozi wa jamii zinazoishi mjini Bor, mji mkuu wa Jonglei, Ajang Bior.
“Utabiri uliopo ni kwamba kati ya sasa na mwezi ujao hali ya maisha itakuwa ngumu kwa watu wetu wanaoishi katika sehemu yenye mvua nyingi na mafuriko, “ ameongeza Ajang Bior .
Jimbo la Jonglei, lina kaunti tatu: Bor, Twic Mashariki na Duk. Jimbo hilo lina watu milioni moja na laki tatu.