Museveni: Nchi za Afrika zinapaswa kuondoa ukomo wa kuwania urais
Mwezi mmoja baada ya Mahakama ya Juu nchini Uganda kuunga mkono hatua ya bunge kuondoa ukomo wa kuwania urais nchini humo, rais Yoweri Museveni anataka mataifa ya Afrika yaondokane na sheria zinazowazuia viongozi wenye umri mkubwa kuwania urais katika nchi zao.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Rais Yoweri Museveni wa Uganda anataka nchi za Afrika kukubali kubadlisha katiba zao kuondoa vizuizi vinavyowakataza viongozi wenye umri mkubwa na wale ambao wametawala kwa muda mrefu kuwania urais.
Rais Yoweri Museveni amesema kwamba ukomo uliowekwa kwenye katiba kama vile ukomo kwa mihula na ukomo kwenye umri vinazuia Afrika kuwa na viongozi wazuri na wenye uzoefu.
Rais Museveni anajiandaa kuwania katika uchaguzi wa urais mwaka 2021 na
akishinda, atakuwa mmoja wa viongozi wa Afrika waliotawala muda mrefu zaidi (miaka 40).
Bunge la Uganda limebadilisha katiba mara mbili na kumpa nafasi Museveni
kuwania kwenye kiti cha urais. Mnamo mwaka 2005, bunge liliondoa ukomo wa mihula na mwaka 2017 likaondoa ukomo wa umri wa miaka 75 nakumpa nafasi
Museveni kuwania kwenye kiti cha urais mwaka 2021.
Rais Museveni alitoa mfano wa nchi ya Tunisia, kuthibitisha kwa nini watu wenye umri mkubwa wanapaswa kuendelea kuwa viongozi kwa nchi za Afrika.
“Ukiwa na mwenye umri mkubwa wa miaka 75 kwa nini unasema aende wakati
anaweza kusaidia? Kuna nchi inayoitwa Tunisia, walifanya mageuzi lakini
walimtafuta mtu mwenye umri mkubwa wa miaka 88. Na huyo ndiye anawasaidia kwa sasa, ” amesema rais Museveni.
Mwanasiasa wa chama cha NRM, Mike Mukul ameunga mkono hoja hiyo ya Museveni na kusema “nchi za Afrika zinapaswa kuzingatia nasaha ya rais Museveni”.
“Mambo ambayo Rais Museveni ametaja ni lazima tuanze kuyafikiria kama Waafrika sababu ukiangalia nchi ambazo zimeendelea, hawana ukomo kwenye
katiba zao, ” amesema Mike Mukula.
Hata hivyo kauli hii ya Museveni imefutiliwa mbali na upinzani nchini Uganda, ukisema kuwa kauli hiyo inapotosha.
"Kauli hiyo ni potofu kwa sababu itasababisha nchi nyingi Afrika kuongozwa na watu ambao wataendelea kusalia madarakani, na iwapo watafariki, dunia kuna hatari familia zao kuendelea kutawala, jambo ambalo halikubaliki, “ amesema Gawaya Tegule, mwanasiasa wa upinzani ambeye pia ni mwanasheria.
Watataalam kuhusu mambo ya utawala wanasema viongozi wakisalia muda mrefu madarakani wanapaswa kujihusisha na upendeleo, rushwa na ukiukwaji wa haki za binadamu.
Kauli hii ya Museveni inakuja wakati huu nchi nyingi barani Afrika zinakabiliwa na maandamano ya kiraia kushinikiza viongozi wao kuachia ngazi.