Pata taarifa kuu
BURUNDI-SIASA-KATIBA

Warundi wajitokeza kuipigia kura marekebisho ya Katiba

Raia wa Burundi wanaokadiriwa kuwa Milioni 4.8  wanapiga kura kuamua kuifanyia mabadiliko Katiba au kupinga mabadiliko hayo, katika zoezi linaendelea kwa utulivu lakini kwa hofu miongoni mwa raia wa nchi hiyo ya Afrika ya Kati.

Wananchi wa Burundi, wafuasi wa chama tawala CNDD FDD
Wananchi wa Burundi, wafuasi wa chama tawala CNDD FDD © STR / AFP
Matangazo ya kibiashara

Iwapo mabadiliko hayo yatafanyika, huenda rais Pierre Nkurunziza akaamua kuwania urais mwaka 2020 na kuendelea kuwa madarakani hadi mwaka 2034.

Wanajeshi na Polisi wameonekana wakipiga doria katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo, hasa jijini Bujumbura kuhakikisha kuwa wapiga kura bila wasiwasi.

Mamia ya wapiga kura wameonekana katika mistari mbalimbali kuanzia saa 12 asubuhi saa za Afrika ya Kati. Tume ya Uchaguzi imesema zoezi la kupiga kura litamalizika saa 10 jioni.

Wananchi wa Burundi wanaamua kati ya ndio (Ego) au la (Oya) kuhusu hatima ya Katiba hiyo.

“Foleni ndefu ya wapiga kura imeonekana jijini Bujumbura.Raia wa Burundi walikuwa na hamu ya kupiga kura,” amesema msemaji wa rais Nkurunziza, Willy Nyamitwe kupitia ukurasa wake wa Twitter.

“Nimekuja mapema kupiga kura ya ndio ili kuthibitisha uhuru wa nchi yetu,” alisema Mkulima aliyejiita Miburo akiwa katika mji wa Ngozi.

Burundi ilifikaje hapa ?

Serikali ya Burundi ilipata wazo la kuibadilisha Katiba ya nchi hiyo baada ya jaribio la mapinduzi ya kijeshi dhidi ya rais Piere Nkurunziza mwaka 2015 ambalo halikufanikiwa.

Haya yote yalikuja, baada ya rais Nkurunziza kutangaza kuwa angewania urais kwa muhula wa tatu licha ya pingamizi kutoka kwa wapinzani wake.

Upinzani ulisisitiza kuwa rais Nkurunziza alikuwa amehudumu kwa mihula miwili na muda wake wa kuondoka ulikuwa umefika kwa mujibu wa katiba na mkataba wa amani wa Arusha.

Hata hivyo, Nkurunziza alisema muhula wake wa kwanza ulianza mwaka 2010 wala sio mwaka 2005 kwa sababu, wakati huo alichaguliwa na wabunge wala sio wananchi.

Watu 1,200 walipoteza maisha katika mzozo wa kisiasa uliochukua miezi kadhaa, huku wengine wakikamatwa na wengine kutoweka.

Wanasiasa wa upinzani, wanahabari na wanaharakati waliikimbia nchi hiyo kwa hofu ya kukamatwa au kuuawa na maafisa wa usalama.

Mwezi Julai mwaka 2016, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio la kuwatuma polisi 228 wa Kimataifa nchini humo lakini serikali ya Burundi ilikataa.

Katika kipindi hicho pia, Burundi ilitangaza kuwa inajiondoa kwenye Mahakama ya Kimataifa ya ICC baada ya kushtumiwa kuwa inakiuka haki za binadamu.

Kuelekea upigaji kura hapo kesho, mamia ya wapinzani wa rais Nkurunziza bado wanazuiwa na mapema mwezi huu, serikali ya Bujumbura ilitangaza kuzima mitambo ya vituo vya redio vya Kimataifa vya BBC na VOA kwa madai ya kupeperusha taarifa za uongo na zinazotishia usalama wa nchi hiyo huku Radio France International ikionywa.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.