NASA yaanza maandamano ya kushinikiza mabadiliko ndani ya Tume ya Uchaguzi
Wafuasi wa muungano wa upinzani nchini Kenya wamekuwa wakiandamana kushinikiza mabadiliko ndani ya Tume ya Uchaguzi kuelekea Uchaguzi mpya wa urais mwezi ujao.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Maandamano hayo yamefanyika katika jiji kuu la Nairobi, mjini Kisumu, na mjiji ya Magharibi ya nchi hiyo ambayo ni ngome kuu ya upinzani.
Jijini Nairobi, polisi walilazimika kutumia mabomu ya machozi kuwasambaratisha waandamanaji waliokuwa wamekusanyika nje ya Ofisi za Tume ya Uchaguzi baada ya kubainika kuwa, kulikuwa na waandamani wengine waliokuwa wanapinga maandamano ya upinzani.
Kiongozi wa NASA Raila Odinga amesema, maandamano hayo yaliyoanza leo yanalenga kushinikiza mabadiliko ndani ya Tume hiyo na kusisitiza kuwa, hawatashiriki katika Uchaguzi uliopangwa iwapo hakutakuwa na mabadiliko.
“Uchaguzi hautakuwepo iwapo, mabadiliko haya tunayoyashinikiza hayatafanyika,” alisema Odinga akiwa jijini Nairobi.
Maandamano haya yamefanyika licha ya Tume ya Uchaguzi kuomba NASA kutoendelea na maandamano hayo baada ya kuandaa makutano na wadau wote wa siasa siku ya Jumatano.
Moja na masharti ya upinzani ni kujiuzulu kwa Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Uchaguzi Ezra Chiloba ambaye amekiambia kituo cha Runinga nchini humo cha KTN News kuwa hafikirii kujiuzulu.
“Sifikirii hilo, kwa sababu nina kazi kubwa mbele yangu,” alisema Chiloba.
Rais Uhuru Kenyatta pamoja na kusema kuwa anaheshimu maandamano ya wapinzani kwa mujibu wa katiba ya nchi hiyo, amesema kuwa Odinga hana mamlaka ya kushinikiza mabadiliko ndani ya Tume hiyo.
Aidha, amesema iwapo Odinga hataki Uchaguzi, ajiondoe kuelekea Uchaguzi huo mpya uliopangwa.
Baada ya maandamano ya Jumatatu, Wakenya wanajiuliza je, masharti ya upinzani yatatekelezwa ? Wakenya wanasubiri kuona.