Pata taarifa kuu
Tanzania

Mkutano wa 18 wa EAC waendelea jijini Dar es Salaam

Mkutano wa 18 wa wakuu wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki unaendelea jijini Dar es salaam nchini Tanzania baada ya kuahirishwa mara tatu kuanzia mwezi Novemba mwaka jana.

Baadhi ya viongozi wa EAC katika mkutano wa 17 uliofanyika jijini Arusha Tanzania
Baadhi ya viongozi wa EAC katika mkutano wa 17 uliofanyika jijini Arusha Tanzania
Matangazo ya kibiashara

Viongozi hao wanakutana kujadili masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na ushirikiano wa kibiashara kati ya Umoja wa Ulaya na Jumuiya ya Afrika Mashariki, mchakato wa shirikisho la kisiasa na kuiingiza Somalia katika Jumuiya hiyo.

Mwandishi wa RFI anayehudhuria mkutano huo unaofanyika katika Ikulu ya Dar es salaam anasema kuwa masuala mengine yanayojadiliwa ni pamoja na namna ya kufadhili shughuli za jumuiya hiyo, utengenezaji wa magari katika Jumuiya hiyo na upigaji marufuku wa nguo za mitumba zinazoingizwa ndani ya Jumuiya.

Pamoja na hayo, mfumo mmoja wa elimu ya juu katika vyuo vikuu unazinduliwa katika mkutano huo kwa lengo la kuhakikisha kuwa elimu inayotolewa katika vyuo vikuu na utunzaji wa alama unafanana.

Mjumbe kutoka Umoja wa Ulaya ambaye hakutaka jina lake kutajwa ameimbia RFI kuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki ina mipango mizuri lakini sula la utekelezwaji linaendelea kuwa changamoto kubwa.

'Tatizo hapa ni utekelezwaji wa wanayokubaliana kila mmoja anataka kutekeleza maslahi ya nchi yake kwanza, alisema.

Aidha, ameonya kuwa ikiwa hali hii itaendelea, huenda malengo ya Jumuiya hiyo yasifikiwe haraka iwezekavyo.

Suala la mkataba wa kiuchumi kati ya EAC na EPA umeonekana kuwagawa viongozi wa nchi hizo wanaokutana na inasubiriwa kuona ni kitu gani kitakaafikiwa.

Viongozi wanaohudhuria mkutano huu ni pamoja na rais wa Tanzania John Magufuli, rais wa Uganda Yoweri Museveni, Naibu rais wa Kenya William Ruto na wawakilishi wengine kutoka serikali ya Rwanda, Burundi na Sudan Kusini.

Rais Museveni anachukua Unyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kutoka kwa rais Magufuli.

 

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.