Wanasiasa nchini Kenya wachuana vikali katika Uchaguzi wa mchujo ndani ya vyama
Seneta wa Kaunti ya Nairobi nchini Kenya Mike Sonko, anamenyana vikali na aliyekuwa Waziri Peter Kenneth kutafuta mgombea wa chama tawala cha Jubilee kuwania Ugavama katika kaunti hiyo wakati wa Uchaguzi Mkuu mwezi Agosti.
Imechapishwa:
Maelfu ya wafuasi wa Jubilee wamejitokeza kupiga kura katika maeneo mbalimbali ya jiji hilo ili kumpata mgombea atakayepambana na Gavana Evans Kidero anayetetea wadhifa wake kupitia chama cha upinzani cha ODM.
Wakati wa kipindi cha kampeni, mahasimu hao wa kisiasa walikuwa wanatupiana maneno makali huku Kenneth akidaiwa kuungwa mkono na rais Uhuru Kenyatta na wafanyibiashara wakubwa jijini Nairobi, madai ambayo hata hivyo yamekanushwa.
Wakati uo huo, matokeo kutoka vyama vingine kutoka kaunti mbalimbali yameanza kutangazwa na baadhi ya wabunge wa sasa, Maseneta na Magavana kutoka chama tawala na upinzani wameshindwa.
Zoezi hili linakamilika siku ya Jumapili. Ni zoezi ambalo linapima demokrasia ya vyama vya siasa nchini Kenya licha ya kuwepo kwa malalamishi ya wanachama kukosa majina yao katika daftari la kupigia kura lakini pia madai ya wizi wa kura.
Waziri wa Mambo ya ndani Joseph Nkaiserry mapema wiki hii aliwaonya wanasiasa na watu wengine wataozua fujo kipindi hiku cha kisiasa, watachukuliwa hatua kali za kisheria.
Muungano wa upinzani nao siku ya Alhamisi, unatarajiwa kumtangaza mgombea wake wa urais kupambana na rais Uhuru Kenyatta.
Miongoni mwa wanasiasa wanaotafuta tiketi hiyo ya muungano huo wa NASA ni pamoja na aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga, Kalonzo Musyoka, Musalia Mudavadi na Moses Wetangula.