Rwanda kuadhimisha Jumapili miaka 30 ya mauaji ya kimbari
Rwanda inajiandaa kuadhimisha siku ya Jumapili kumbukumbu ya miaka 30 ya mauaji ya Kimbari ya mwaka 1994 ambapo Wahutu wenye msimamo mkali waliwaua watu karibu milioni moja wengi wao wakiwa ni Watutsi.
Imechapishwa:
Vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyoanza April 7 mwaka 1994 na vilivyodumu kwa siku 100, vilishuhudiwa siku moja tu baada ya kudunguliwa kwa ndege aliyokuwamo rais wa wakati huyo wa Rwanda Juvénal Habyarimana pamoja na yule wa Burundi Cyprien Ntaryamira.
Viongozi hao walikuwa wametoka kwenye mkutano wa kilele nchini Tanzania ambako walikuwa wanajadili mzozo huo wa Rwanda. Mauji ya kimbari ya mwaka 1994 ni miongoni mwa matukio mabaya zaidi kuwahi kushuhudiwa nchini Rwanda.
Hadi leo hii, makaburi ya jumla yanaendelea kugundulika katika nchi hiyo yenye watu karibu milioni 14. Viongozi mbalimbali akiwemo aliyekuwa rais wa Marekani wakati wa mauaji hayo Bill Clinton wanatarajia kuhudhuria maadhimisho hayo.
Siku ya Alhamisi Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron alisema kwamba Ufaransa na washirika wake wangeweza kukomesha mauaji ya halaiki lakini hawakuwa na nia ya kufanya hivyo. Tamko la Macron lilikuja miaka mitatu baada ya kukiri jukumu kubwa la Ufaransa mshirika wa karibu wa Rwanda wa Ulaya mwaka 1994 kwa kushindwa kuzuia kuingia kwa nchi hiyo kwenye mauaji.