Tanzania: Idadi ya waliokufa kutoka na mafuriko imeongezeka hadi 60
Nairobi – Waziri mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa Jumatatu, Disemba 4, ameongoza katika kutoa heshima za mwisho kwa watu 63 waliofariki kutokana na maporomoko ya udongo na mafuriko kaskazini mwa nchi hiyo, idade hiyo ikitarajiwa kuongezeka.
Imechapishwa:
Mvua kubwa iliyonyesha mwishoni mwa juma ilisomba magari na kuangusha majengo katika mji wa milimani wa Katesh, ulioko kaskazini mwa mji mkuu Dodoma.
Tumepoteza watu 63 ambao miili yao iko mbele yetu leo. Wanaume 23 na wanawake 40, Majaliwa alisema wakati wa hafla ya kukabidhi mabaki ya wahasiriwa kwa familia zao huko Katesh, akiongeza kuwa watu 116 walijeruhiwa.
Tayari rais Samia Suluhu Hassan amefuta ziara yake huko Dubai kwa ajili ya mkutano wa hali ya hewa COP28 na ameagiza kutumwa kwa vikosi vya usalama vya kitaifa katika eneo hilo kusaidia katika juhudi za uokoaji.
Mkuu wa mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amesema hali ya miundombinu inaendelea kushughulikiwa.
Miundombinu ya upande huu wote wa chini imeharibika, kijiji kile pamoja na vitongoji vyake. Tumeendelea na kazi kubwa sana ya kufanya uokoaji na uzuri ni kwamba barabara sasa hivi zimeanza kufanya kazi vizuri.
Tanzania na majirani zake wa Afrika Mashariki Kenya, Somalia na Ethiopia wanakabiliana na mafuriko makubwa yaliyosababishwa na mvua kubwa inayohusishwa na hali ya El Nino, ikikumbukwa kuwa kati ya Oktoba 1997 na Januari 1998, mafuriko yaliyoenea sana yalisababisha vifo vya zaidi ya 6,000 katika nchi tano za eneo hilo.
Idara ya utabiri wa hali ya hewa inaonya kuwa mvua zitaendelea kunyesha mwezi huu.