Mgawanyiko SPLM/A-IO : Riek Machar avunja ukimya na kulaumu wapinzani wake
Makamu wa kwanza wa rais wa Sudan Kusini, Riek Machar sasa anawashtumu wapinzani wake kwenye jeshi la upinzani la SPLM/A-IO kwa kumwondoa kwenye uongozi wa jeshi hilo kwa sababu hawana nia ya nchi hiyo kupata amani.
Imechapishwa:
Kauli hii ya Machar, imetolewa na uongozi wa chama cha upinzani SPLM-IO ambao unasema Majenerali waliotoa kauli hiyo, hawapo tena kwenye Baraza la Jeshi upande wa upinzani.
Aidha, Machar amesema hatua ya Majenerali hao ni kuzuia jitihada za kuliunganisha jeshi la upinzani na lile la taifa kwa mujibu wa mkataba wa amani uliotiwa saini kati yake na rais Salva Kiir mwaka 2018.
Siku ya Jumatano, Majenerali hao walitangaza kumwondoa Machar katika nafasi hiyo baada ya kumtuhumu kuwa alikuwa anakwenda kinyume na maono ya upinzani kwenye serikali ya mpito na sasa nafasi yake imechukuliwa na Jenerali Simon Gatwech Dual.
Watalaam wa masuala ya Sudan Kusini, wanaonya kuwa,kuwepo kwa makundi mawili ya jeshi la upinzani kutarudisha nyuma jitihada za upatikanani wa amani ambazo zilikuwa zimeanza kushuhudiwa katika taifa hilo ambalo mwezi Julai lilitimiza miaka 10 ya uhuru.