Raia wa Sudan Kusini kuadhimisha miaka 10 ya uhuru wakiwa nyumbani
Baraza la Mawaziri nchini Sudan Kusini limeamua kuwa, hakutakuwa na maadhimisho rasmi ya miaka 10 ya kusherehekea uhuru wa taifa hilo changa duniani, kwa hofu ya kusambaa kwa maambukizi ya virusi vya corona.
Imechapishwa:
Kuapishwa kwa wabunge wa bunge jipya la mpito pia kumeahirishwa kutoka siku ya Ijumaa hadi wakati mwingine.
Uamuzi huu umekuja baada ya kikao kisichokuwa cha kawaida kuongozwa na rais Salva Kiir siku ya Jumatano na ikakubaliwa kuwa, wananchi waadhimishe siku hiyo wakiwa majumbani mwao.
Naibu Waziri wa Habari nchini humo Baba Medan hata hivyo ametangaza rais Kiir atawahotubia wananchi wa taifa hilo kupitia Televisheni.
Miaka 10 baada ya Sudan Kusini kupata uhuru wake kutoka kwa Sudan, baada ya vita vya miaka 21, nchi hiyo bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali hasa vita kati ya makundi ya waasi na jeshi la serikali, mapigano ya kikabila, baa la njaa miongoni mwa mambo mengine.
Muda mfupi baada ya kuanza kujitawala wanasiasa nchini humo rais Kiir na Makamu wa kwanza wa rais Riek Machar walianza kuzozana na kusabababisha vita mpaka 2016 wakati pande mbili zilipopata mkataba wa amani kwa usaidizi wa Jumuiya ya Kimataifa.
Mkataba huo haukutekelezwa ipasavyo na vita vikaendelea hadi upatikanaji wa mkataba mpya wa amani uliotiwa saini mwaka 2018 na kuwezesha kuunda serikali ya mpito.