Viongozi wa Sudan na Sudan Kusini wafikia makubaliano kuhusu uzalishaji wa mafuta
Viongozi wa Sudan na Sudan Kusini wameelezwa kufikia makubaliano kuhusu suala la mafuta ambalo litashuhudia uzalishaji wa nishati hiyo toka Sudan Kusini kupitia Khartoum ukianza.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Msemaji wa pande zote mbili ambazo zinakutana mjini Addis Ababa Ethiopia, amethibitisha kufikiwa kwa makubaliano kwenye eneo la mafuta huku masuala mengine ya kiusalama kwenye mpaka wa nchi hizo mbili yakiendelea kuwa kitendawili.
Rais wa Sudan Omar al-Bashir na mwenzake wa Sudan Kusini Salva Kiir wanatarajiwa kutia saini makubaliano hayo hii leo kumaliza mvutano uliokuwepo kuhusu ugawanaji wa mafuta kutoka jimbo la Abyei.
Licha ya kufikia makubaliano hayo bado taarifa za kina kuhusu uzalishaji huo wa mafuta hazijatolewa ingawa inaelezwa kuwa uzalishaji wa nishati hiyo utaanza mara moja mara baada ya viongozi hao kutiliana saini.
Masuala kadhaa yameendelea kuwa kitendawili ikiwemo suala la kimipaka hasa kwenye eneo la Abyei ambapo viongozi hao bado hawajakubaliana, huku suala la mataifa hayo kuondoa majeshi yao kwenye mipaka likielezwa kupatiwa suluhu ya muda.
Makubaliano hayo yanafikiwa wakati ambapo Umoja wa Mataifa umetishia kuziwekea vikwazo nchi hizo iwapo zitashindwa kumaliza tofauti zao za kimipaka na usalama kwenye maeneo yao.
Kufikiwa makubaliano kwa suala la Mafuta kutafanya mataifa hayo kugawana shea sawa kutokana na uzalishaji wa mafuta ambao ulisimama baada ya kutokea kutokuelewana kuhusu ugawanaji wa fedha za mauzo ya mapipa ya mafuta.