Pata taarifa kuu
HAITI-HAKI

Haiti: Waziri Mkuu amfuta kazi mwendesha mashtaka aliyedai kumfungulia mashitaka

Bed-Ford Claude, mwendesha mashtaka mkuu wa Port-au-Prince, Jumanne, Septemba 14, aliomba jaji anayechunguza mauaji ya rais Jovenel Moïse kumfungulia mashitaka Waziri Mkuu.

Waziri Mkuu wa Haiti Ariel Henry, Julai 20, 2021 huko Port-au-Prince.
Waziri Mkuu wa Haiti Ariel Henry, Julai 20, 2021 huko Port-au-Prince. AP - Joseph Odelyn
Matangazo ya kibiashara

Kulingana mwendesha mashtaka mkuu wa Port-au-Prince, Ariel Henry anadaiwa aliwasiliana kwa njia ya simu na mmoja wa washukiwa wakuu wa mauaji hayo. Katika mchakato huo, waziri Mkuu Ariel Henry ameamua kumfuta kazi.

Baada ya kifo cha rais wa Haiti Jovenel Moïse, aliyeuawa kwa kupigwa risasi nyumbani kwake huko Port-au-Prince na kundi la watu wenye silaha mnamo Julai 7, Bed-Ford Claude alituma barua kwa mahakama ya kwanza katika mji mkuu Jumanne wiki hii. Katika barua yake hiyo, kamishna wa serikali - wadhifa sawa na ule wa mwendesha mashtaka -, alimuomba jaji anayesimamia uchunguzi wa mauaji ya rais Jovenel Moise kumshtaki Waziri Mkuu, Ariel Henry.

Kuna "ushahidi wa kutosha" unaofanya Bwana Henry kufikishwa mahakamani na kufunguliwa mashitaka", aliandika Bed-Ford Claude, ambaye tayari alikuwa amemwalika kiongozi wa serikali siku ya Ijumaa wiki iliyopita kuripoti kwenye ofisi ya mashtaka Jumanne wiki hii. Alikuwa amedai kwamba Ariel Henry alifanya mazungumzo ya simu na Joseph Félix Badio, mmoja wa watu wanaosakwa kuhusiana na uchunguzi wa mauaji ya Jovenel Moïse. Mazungumzo haya inasemekana yalifanyika saa kadhaa baada ya kifo cha rais.

Kamishna wa serikali pia aliomba Ariel Henry kutotoka nchini

Simu ya Joseph Félix Badio ilionekana katika eneo ambalo kunapatikana makazi ya kibinafsi ya Jovenel Moïse alipomuita kwa simu Ariel Henry saa 04:03 na 04:20, usiku wa shambulio hilo. Siku ya Jumamosi, Waziri Mkuu alipuuzilia mbali shutuma hizi akisema: "Ujanja wa kupindukia ili kuzusha mkanganyiko na kuzuia vyombo vya sheria kufanya kazi yake kwa utulivu hauna nafasi!" Wahusika wakuu wa mauaji ya Jovenel Moïse, na wadhamini wa mauaji hayo, watapatikana, watafikishwa mahakamani na kuadhibiwa kwa uhalifu wao. "

Licha ya utetezi wa Ariel Henry, siku ya Jumanne Bed-Ford Claude alidomba Waziri Mkuu azuiliwe kuondoka nchini Haiti "kwa sababu ya uzito wa ukweli ulio wazi". Katika barua ya pili, aliyomuandikia Mkuu wa mamlaka ya Uhamiaji , alitetea ombi hili la kuzuiwa kwa  Ariel Henry kuondoka nchini Haïti "kwa tuhuma nzito za mauaji ya rais wa Jamhuri".

Kufuatia ombi hilo la kufunguliwa mashtaka, Ariel Henry alichukuwa uamuzi wa kumfuta kazi Bed-Ford Claude saa machache baadaye.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.