CAR: Kumi na moja wauawa katika shambulio la waasi Bambari
Watu 11 wameuwa nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, baada ya kuvamiwa na waasi, wakati huu mapambano yakiendelea kati ya makundi yenye silaha Mashariki mwa nchi hiyo na vikosi vya usalama.
Imechapishwa:
Mashambulizi dhidi ya raia yalitokea karibu na mji wa Bambari, wakati magari yaliposhambuliwa na kusababisha maafa ya raia hao na wengine sita wakaachwa na majeraha.
Hata hivyo afisa mwingine wa serikali katika eneo hilo amesema ,idadi ya watu walipoteza maisha ni 15.
Mji wa Bambari ulio umbali wa Kilomita 380 kutoka mji mkuu Bangui, umeendelea kusumbuliwa na waasi wanaojiita UPC, ambao hivi kairbuni waliwauwa wanajeshi wawili wa serikali.
Hali ya usalama imeendelea kuwa mbaya katika nchi hiyo, na kuanzia tarehe moja mwezi Oktoba, serikali ilitangaza kuongeza muda wa watu kutotembea nje.
Tangu mwaka 2013, taifa hilo limeendelea kushuhudia utovu wa usalama baada ya aliyekuwa kiongozi w anchi hiyo Francois Bozize, kuondolewa madarakani na waasi.