DRC: Mwanaharakati wa pili wa Lucha akamatwa
Mwanaharakati mwingine wa vuguvugu linaloshinikiza mabadiliko nchini DRC Lucha, amekamatwa baada ya vuguvugu hili kumshtumu mke wa rais Félix Tshisekedi kutofikisha msaada wa chakula kwa watu waliothirika na mlipuko wa Volkano Mashariki mwa nchi hiyo mwezi Mei.
Imechapishwa:
Ghislain Muhiwa, anakuwa mwanaharakati wa pili wa Lucha, kukamatwa na maafisa wa usalama na alikamatwa nyumbani kwake jana mchana kwa mujibu wa ndugu zake.
Baada ya kukamatwa, alipelekwa kwenye kambi ya jeshi, katika mkoa wa Kivu Kaskazini.
Muhiwa anadaiwa kumharibia jina wakfu wa Denise Nyakeru Tshisekedi, baada ya kudai kupitia ukurasa wa Twitter wa Lucha, Juni 4, wakfu huo haukuwasilisha msaada uliotakiwa kuwasaidia waliothiriwa na mlipuko wa volkano.
Mwaharakati wa Kwanza kukamatwa ni Parfait Muhani aliyetiwa mbaroni Julai 7, huku mwingine akiendelea kusakwa.
Vuguvugu la Lucha liliundwa mwaka 2012 mjini Goma kwa lengo la kuwaajibisha viongozi wa DRC.