Pata taarifa kuu
BURKINA FASO-MAUAJI-USALAMA

Shambulio Burkina: Raia 35 wauawa, ikiwa ni pamoja wanawake wengi

Raia thelathini na tano, ikiwa ni pamoja na wanawake 31, wameuawa Jumanne katika shambulio la wanajihadi lililotokea katika mji wa Arbinda, Kaskazini mwa Burkina Faso.

Gari la eshi la Burkina Faso likipiga doria katika mkoa wa Soum, Novemba 2019.
Gari la eshi la Burkina Faso likipiga doria katika mkoa wa Soum, Novemba 2019. © MICHELE CATTANI / AFP
Matangazo ya kibiashara

Shambulio hilo baya kuwahi kutokea katika historia ya nchi hiyo ya ukanda wa Sahel linaendelea kuonyesha mdodroro wa usalama katika ukanda huo.

Serikali ya Burkina Faso imetangaza saa 48 ya maombolezo ya kitaifa.

Rais wa Burkina Faso mwenyewe, Roch Kaboré , ambaye mara kadhaa amekuwa akikosolewa kushindwa kuyadidimiza makundi ya kijihadi, ndiye ametangaza kwenye ukurasa wake wa Twitter idadi hiyo ya kutisha ya "shambulio hilo la kikatili".

Wanajeshi wanne na maafisa watatu wa polisi pia wameangamia katika shambuliohilo, na 'magaidi 80 wameuawa' , kwa mujibu wa rais na uongozi wa majeshi ya Burkina Faso, ambao ulitangaza shambulio hilo mapema katika taarifa.

Siku ya Jumanne asubuhi, "idadi kubwa ya magaidi walishambulia kwa wakati mmoja askari na raia wa Arbinda", katika mkoa wa Soum, kwa mujibu wa uongozi wa majeshi. Shambulio 'kubwa', lililodumu 'saa kadhaa'.

'Katika kukimbia kwao, magaidi hao waliwaua kikatili raia 35, wakiwemo wanawake 31, na kuwajeruhi watu sita," waziri wa mawasiliano na msemaji wa serikali Remis Dandjinou amesema katika taarifa yake Jumanne jioni.

Askari "ishirini" pia wamejeruhiwa, waziri huyo ameongeza.

Ni moja ya mashambulio mabaya kuwahi kuikumba nchi hii maskini ya Afrika Magharibi, ambayo inaendelea kukabiliwa na mashambulizi ya kijihadi tangu mwaka 2015, kama majirani zake Mali na Niger.

Mwanzoni mwa mwezi Novemba, wafanyakazi 38 wa kampuni moja ya madini waliuawa wakati wa shambulio dhidi ya msafara wao Mashariki mwa nchi.

- Jeshi lakabiliwa na uhaba wa vifaa -

Rais Kaboré amesifu 'kujitolea na ushujaa' wa vikosi vya ulinzi na usalama, ambavyo 'vilizima shambulio dhidi ya kambi ya jeshi la Arbinda". "Pikipiki kadhaa, silaha nyingi na risasi pia vimerejeshwa,' kwa mujibu wa uongoi wa majeshi.

Tangu mwaka 2015, mashambulizi ya wanajihadi nchini Burkina yamewauwa watu zaidi ya 700, kulingana na takimu za shirika la habari la AFP, na karibu watu 560,000 wameyatoroka makazi yao, kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.