Pata taarifa kuu
DRC-MONUSCO-USALAMA

Sherehe ya kuaga askari wa Tanzania waliouawa DRC yafanyika leo Alhamisi Dar es Salaam

Miili ya wanajeshi 14 wa Tanzania waliouawa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wiki iliyopita imeagwa leo jijini Dar es salaam katika tukio lililohudhuriwa na watu mbalimbali wakiwemo viongozi wa serikali, maofisa kutoka Umoja wa Mataifa na wananchi.

Askari wa Tanzania wakipokea miili ya askari wa MONUSCO kutoka Tanzania waliouawa Beni, DRC, Dar es Salaam, Desemba 11, 2017
Askari wa Tanzania wakipokea miili ya askari wa MONUSCO kutoka Tanzania waliouawa Beni, DRC, Dar es Salaam, Desemba 11, 2017 REUTERS/Emmanuel Herman
Matangazo ya kibiashara

Huzuni, majonzi na simanzi vimetawala wakati mamia kwa maelfu ya wakazi wa jiji la Dar es salaam walipojitokeza katika Uwanja wa Ngome uliopo makao makuu ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania, kuaga miili ya askari 14 waliouawa Disemba nane wakati wakilinda amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo

Akizungumza na RFI Kiswahili, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa wa Tanzania Dr. Hussein Mwinyi amesema umefika wakati kwa Umoja wa Mataifa kutoa nguvu kwa majeshi ya kulinda amani.

Katika sherehe hiyo iliyofanyika jijini Dar es Salaam, alikuepo Mkuu wa wa shughuli za kulinda amani kwenye Umoja wa Mataifa, Jean-Pierre Lacroix. Siku ya Ijumaa, Bw Lacroix anatarajiwa kusafiri kwenda Goma kwa ajili ya sherehe mpya kwa wahanga hao. Wakati huo huo uchunguzi wa ndani kwenye Umoja wa Mataifa unaendelea ili kuelewa vizuri mazingira ya shambulio hilo.

Miili ya askari hao imesafirishwa kuelekea mikoa ya Shinyanga, Mtwara, Rukwa, Kagera, Dodoma na Zanzibar kwa ajili ya mazishi.

Ushahidi uliokusanywa na RFI

Kabla ya saa 11:30 joni, muda mfupi kabla ya usiku, kundi la kwanza la washambuliaji liliingia katika kambi wakijifananisha kama askari wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (FARDC). Mavazi yao yalifanana na sare za jeshi la DRC (FARDC), walikua wakiongea Kiswahili na walisema kuwa wanaleta chakula katika kambi hiyo, vyanzo kadhaa vimeeleza, hali ambayo ilikua ni kama mazoewea katika kambi hiyo.

Wakati huo huo, washambuliaji wengine, ambao walikua wengi, walipiga kambi katika msitu mdogo upande wa pili wa barabara. Muda mchache baadae, risasi za kwanza zilifyatuliwa katika kambi hiyo. Risasi hizo zilikua zikitokea ndani na nje ya kambi. Papo hapo washambuliaji walifahamu sehemu kulipokua mitambo ya mawasiliano na walifanikiwa kuizima. Kulingana na ushahidi uliokusanywa na RFI, mitambo hiyo haikuharibiwa, lakini ilipelekwa na washambuliaji, sawa na silaha pamoja na vifaa vingine vya kijeshi vilivyoachwa katika eneo hilo, chanzo cha kijeshi kimebaini.

Uchunguzi unaendelea

Kuhusu muda wa mapigano, taarifa mbili zimetofautiana. Masaa 4, kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, masaa 13 kwa mujibu wa kikosi cha jeshi la Tanzania. Vyanzo vingine vinasema kutokana na nguvu walizokua nazo washambuliaji, askari wa Tanzania walikimbilia haraka, huku wakiacha kambi yenyewe, magari kadhaa yakichomwa moto. Mpaka sasa haijafahamika rasmi aliyehusika na shambulio hili. Na bado ni vigumu kuelezea hali halisi ya mambo. Ikiwa kweli kutakua na taarifa ya kuthibitishwa kwamba waasi wa Uganda wa ADF ndio walitekeleza shambulio hilo, basi itaonekana kuwa kundi hili lina wapiganaji wengi ambao wana silaha za kutosha na wana mafunzo ya kutosha.

Miongoni mwa askari watatu waliotoweka siku moja baada ya shambulio hilo, wawili walipatikana siku ya Jumamosi iliyopita. Askari mmoja wa kikosi cha Umoja wa Mataifa bado anakosekana, na zoezi la kumtafuta linaendelea, kwa mujibu wa chanzo cha Umoja wa Mataifa. Jeshi la DRC pia limeanzisha uchunguzi ili kufahamu mazingira ya shambulio hilo.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.