Upinzani nchini DRC unatafuta Mwenyekiti mpya wa Kamati ya wazee wa Busara
Viongozi wa siasa kutoka chama cha upinzani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo UDPS, wajadili upatikanaji wa Mwenyekiti mpya wa Kamati ya wazee wa busara baada ya kifo cha Ettiene Tshisekedi.
Imechapishwa:
Naibu Katibu Mkuu wa chama cha UDPS Bruno Tshibala, amesema ataongoza Kamati ya kumpata Mwenyekiti mpya kamati ambayo itakuwa na kazi ya kuhakikisha kuwa mkataba wa kisiasa wa mwaka 2016 unatekelezwa kikamilifu.
Hatua hii imechukuliwa baada ya Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki CENCO lililoongoza upatikanaji wa mkataba huo kutaka kupatikana kwa Mwenyekiti mwingine ili kuendelea kwa majadiliano ya utekelezwaji wa mkataba huo wa kisiasa.
Chama cha UDPS kinataka kuteuliwa kwa Waziri Mkuu na kuanza kufanya kazi kwa serikali ya mpito kabla ya mwili wa Tshisekedi kurejea nyumbani na kuzikwa.
Kwa mujibu wa mkataba huo, Uchaguzi Mkuu nchini DRC unatarajiwa kufanyika mwisho wa mwaka huu.
Hata hivyo, serikali ya Kinshasa imeonekana kutokuwa na uhakika wa Uchaguzi huo baada ya Wizara ya Fedha kusema haina fedha za kufanikisha zoezi hilo.