Mji wa Kinshasa wakumbwa na machafuko
Mji wa Kinshasa umeendelea kushuhudiwa machafuko, baada ya hali ya utulivu kuripotiwa Jumatano Januari 19 jioni.
Imechapishwa:
Polisi imefyatua risasi hewani ili kuwatawanya waandamanaji ambao walikua wakiandamana dhidi ya muswada wa sheria ya uchaguzi, ambao unatoa nafasi ya kuahirisha uchaguzi wa urais uliopangwa kufanyika mwaka 2016. Vikosi vya usalama na waandamanaji wamekua wakichukuliana kama maadui.
katika maeneo mbalimbali ya mji wa Kinshasa, makabiliano yameendelea kushuhudiwa kati ya polisi na waandamanaji. Karibu na chuo mjini Kinshasa, kundi la wanafunzi hamsini wamezuia barabara kwa kuchoma matairi, huku kikosi cha kuzima fujo kikifyatua risasi hewani ili kuwatawanya wanafunzi hao.
Machafuko yameendelea kushuhudiwa katika maeneo mbalimbali. Barabara itokayo kwenye mabweni ya chuo kikuu yamezuiliwa mapema leo Jumanne Januari 20. Vitu vya aina mbalimbali vimekua vimewekwa barabarani kama vizuizi kwa magari. Polisi imetumia mabomu ya kutoa machozi kwa kuwatawanya waandamanaji, na watu kadhaa wamekamatwa.
Ni vigumu kutabiri hali ilivyo katika mji wa Kinshasa, kwani makundi ya watu yamekua yakijitokeza pale polisi inapofika sehemu.
Viongozi kadhaa wa vyama vya upinzani wamekamatwa. Jean-Claude Muyambo, kutoka upinzani, ambaye awali alikua upande wa chama tawala cha PPRD, amekamatwa. Hata kiongozi wa chama cha MMP, Franck Diongo amewekwa ndani.