Ukraine: Kongamano la kwanza la kimataifa la viwanda vya ulinzi lafunguliwa Kyiv
Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amefungua kongamano la kwanza la kimataifa la viwanda vya ulinzi jijini Kyiv, akiwa na nia ya kuvutia watengenezaji zaidi wa silaha nchini Ukraine.
Imechapishwa:
Kyiv imekuwa ikitegemea sana misaada ya nchi za Magharibi tangu Urusi ilipovamia mwaka jana, lakini inazidi kutaka kuimarisha sekta yake ya silaha za ndani huku kukiwa na hofu kwamba uungwaji mkono kutoka kwa washirika wake huenda ukayumba.
Rais Zelensky amesema kwa sasa lengo ni kushinda vita kati yake na Urusi na kurejesha amani ya kudumu kwa raia wake.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari wakati wa hafla hiyo, kiongozi huyo amesema mpango huo utafanikishwa kwa ushirikiano na watu wote.
Maafisa kutoka zaidi ya nchi 30 na mashirika 250 katika sekta ya ulinzi walikusanyika kwa ajili ya kongamano hilo, ambalo linakuja wakati Zelensky akizishawishi nchi za Magharibi kupata silaha zaidi ili kufanya mashambulio dhidi ya Urusi.
Kyiv ilizindua harakati zake za kuchukua tena maeneo yake yanayokaliwa na Urusi mwezi Juni ambapo imekuwa ikiripoti mafaniko madogo katika uwanja wa mapambano huku wanajeshi wake wakikabiliana na ulinzi wa Urusi ulioimarishwa zaidi.
Haya yanajiri wakati huu maafisa wa Ukraine wakisema kuwa jeshi la anga la nchi hiyo lilidungua ndege 30 zisizo na rubani za Shahed zilizotengenezwa na Iran zilizorushwa na Urusi katika shambulio la usiku katika eneo la kati la Vinnytsia na maeneo ya kusini ya Odesa na Mykolaiv.