Paka wamethibitishwa kuambukizwa homa ya ndege Poland
Nairobi – Poland imekuwa nchi ya kwanza kuripoti "idadi kubwa" ya paka walioambukizwa homa ya ndege katika eneo kubwa, kwa mujibu wa shirika la afya duniani WHO.
Imechapishwa:
Licha ya ripoti hiyo, hatari ya binadamu kuambukizwa homa hiyo bado ipo chini.
Kwa mujibu wa WHO, tangu idara ya afya nchini Poland mwezi uliopita kuripoti vifo vya paka visivyo vya kawaida kote nchini, paka 29 walipatikana na homa ya ndege ya H5N1.
Paka hao walikuwa miongoni mwa 46 na mnyama mwengine aliyekamatwa ambao walifanyiwa vipimo vya homa hiyo ambapo 14 kati yao waliokuwa wameambukizwa waliuawa na wengine 11 kufariki. Kwa mujibu wa ripoti, paka wa mwisho ambaye alikuwa ameambukizwa alifariki mwezi Juni tarehe 30.
WHO inasema uchunguzi unaendelea kubaini chanzo cha paka hao kuambukizwa homa hiyo.
Baadhi ya paka hao walioambukizwa walionyesha dalili za juu ikiwemo kukabiliwa na changamoto ya kupumua, kuharisha, kuishiwa nguvu na hatimaye kufariki.
Tangu mwishoni mwa mwaka wa 2021, bara Europa limekuwa likabiliwa na viwango vya juu vya homa ya ndege wakati ambapo Marekani ya kaskazini na kusini pia zikiripoti maambukizi.
Kutoka mwaka wa 2020, WHO imepokea ripoti 12 za visa vya maambukizi ya homa ya ndege aina ya H5N1 kote ulimwenguni. Nne kati yao zikiwa kesi mbaya zaidi, wakati nane zilikuwa nyepesi au zisizo na dalili.