Ulaya : Nyuzi za juu za Joto zapungua
Hali ya joto kwenye baadhi ya mataifa ya Ulaya imepungua hivi leo wakati huu wafanyakazi wazimamoto wakijaribu kuudhibiti moto unaoendelea kuunguza mamia ya hekari za misitu kwenye ukanda wa magharibi mwa ulaya.
Imechapishwa:
Haya yanajiri wakati huu nchi ya Uingereza ambayo imekuwa haishuhudii joto la hali ya juu, safari hii imerekodi idadi ya juu zaidi ya kiwango cha joto kilichovuka nyuzi joto 40 kwa mara ya kwanza kwenye historia yake.
Nchi za Ujerumani na Ureno kwa upande wao zimerekodi ongezeko kubwa la joto kuwahi kushuhudiwa kwenye mataifa hayo, pamoja na vifo vya watu kadhaa.
Hapo jana, shirika la kimataifa la hali ya hewa duniani, lilionya kuhusu hali hii kushuhudiwa kwa miongo kadhaa ijayo, ikizitaka nchi kuendelea kuchukua hatua za kusaidia wananchi wao kukabiliana na hali ya joto.
Katika hatua nyingine, wafanyakazi wazimamoto kwenye nchi za Ufaransa na Ugiriki, wameendelea kuukabili moto unaoendelea kutishia maisha ya wakazi walio jirani na maeneo ya misiti inayoteketea, huku watu zaidi ya elfu 35 wakiwa wamehamishiwa sehemu salama.