Vita nchini Ukraine: Washington ‘haina uhakika’ kwamba Urusi imebadilisha mkakati
Urusi imeanza "operesheni yake ya kijeshi", iliyoelezewa kama vita na mataifa mengi ya kigeni, siku 31 sasa. Jumamosi hii, Machi 26, Rais wa Marekani Joe Biden anaendelea na ziara yake barani Ulaya, huku jeshi la Urusi likilazimika kutia kambi na kuendeleza mashambulizi yake mashariki mwa Ukraine, kulingana na maneno yake yenyewe.
Imechapishwa:
Emmanuel Macron, rais wa Ufaransa, kwa upande wake amesema kuwa "zoezi la kipekee la kiutu" linatayarishwa, pamoja na Uturuki na Ugiriki, kuwahamisha raia kutoka mji wa Mariupol unaozingirwa na jeshi la Urusi. Zoezi hili linapaswa kufanyika katika siku chache zijazo. Rais Macron pia amesema kuwa atakuwa na "mazungumzo mapya" na Vladimir Putin, Rais wa Urusi, "ndani ya saa 48 hadi 72".
Vikosi vya Kyiv vimeanzisha mashambulizi dhidi ya mji wa Kherson. Afisa mkuu wa Pentagon anathibitisha hili. "Hatuwezi kusema ni nani hasa anayedhibiti Kherson, lakini ukweli ni kwamba jiji hilo haliko chini ya udhibiti wa Urusi kama hapo awali. "
Katika hatua nyingine Rais wa Marekani Joe Biden amewasili Poland. Ametembelea jeshi la Marekani lililoko nchini humo. Hii ni hatua ya pili baada ya ziara yake mjini Brussels, iliyolenga kuimarisha umoja wa nchi za Magharibi dhidi ya uvamizi wa Urusi nchini Ukraine, katika nyanja ya kidiplomasia na kiuchumi.Rais
Biden amekutana na mawaziri wawili wa Ukraine nchini Poland kuonesha uungaji mkono wa Washington kwa serikali mjini Kyiv wakati Urusi ikiashiria kwamba inaweza kupunguza malengo yake ya kivita nchini Ukraine. Kulingana na wizara ya mambo ya kigeni ya Marekani, mkutano huo kati ya Biden na mawaziri wa mambo ya nchi za nje na ulinzi wa Ukraine ulijikita kwenye kusisitiza dhamira ya Marekani katika kutetea uhuru na hadhi ya mipaka ya Ukraine.