Vita nchini Ukraine: Rais Erdogan ajaribu kuwa mpatanishi kati ya Zelensky na Putin
Rais wa Uturuki, ambaye anajaribu kuchukua nafasi ya upatanishi kati ya Urusi na Ukraine, amebaini kuwepo na maendeleo katika mazungumzo kati ya mahasimu hao wawili.
Imechapishwa:
Katika mahojiano na waandishi wa habari wa Uturuki baada ya mkutano wa kilele wa NATO, ambapo alishiriki Alhamisi Machi 25, Recep Tayyip Erdogan alibaini kuwepo kwa "maelewano" kuhusu pointi nne kati ya sita.
Rais wa Uturuki amebaini kwamba mazungumzo hayo yanaendelea, lakini bado yamezuiwa katika masuala mawili. Kulingana na maneno yaliyotumiwa na Recep Tayyip Erdogan, Kyiv na Moscow "wanaonekana kufikia makubaliano" kuhusu pointi nne.
Kwanza kuhusu kukataa kwa Ukraine kujiunga na NATO, kisha kutambuliwa kwa Kirusi kama "lugha rasmi", Ukraine kutokuwa na silaha kubwa za kivita - ombi la Urusi ambalo Kyiv Itakuwa tayari kwa "makubaliano" - na hatimaye, makubaliano ya "usalama wa pamoja" kwa Ukraine, ambayo Uturuki inaweza kuwa mmoja wa wadhamini.
Hakuna makubaliano kuhusu Crimea na Donbass
Kinyume chake, Kyiv na Moscow bado hazijaweza kukubaliana juu ya hali ya Crimea na Donbass, ambapo Vladimir Putin anadai kutambuliwa kwa "uhuru" wa Urusi. Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky alitangaza kwamba maelewano yoyote juu ya maeneo haya yatalazimika kuidhinishwa na Waukraine katika kura ya maoni.
Rais wa Uturuki anatarajiwa kukutana Ijumaa hii, Machi 25, na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky, kisha tena kwa njia ya simu na mwenzake wa Urusi wikendi hii au mapema wiki ijayo. Atamwita, anasema, kuwa "mtetezi amani" na "kufanya ishara ya heshima", akitumia hapa neno ambalo linaweza kueleweka pia kama wito kwa rais wa Urusi "kuondoka kwa heshima" nchini Ukraine.