Mahamat Idriss Déby azuru Ufaransa kukutana na rais Macron
Mahamat Idriss Déby rais wa Chad yupo nchini Ufaransa anakokutana na mwenyeji wake Emmanuel Macron kujadiliana kuhusu masuala mbalimbali yenye maslahi kati ya nchi hizo mbili.
Imechapishwa:
Taarifa kutoka Ikulu ya Élysée, imesema viongozi hao wawili watazungumzia hali ya siasa nchini Chad, kuelekea uchaguzi ujao.
Mbali na hilo, Emmanuel Macron na Mahamat Idriss Déby Itno watajadiliana pia kuhusu hali ya usalama katika ukanda wa G5 Sahel. Mataifa ya G5 Sahel ni pamoja na Burkina Faso, Chad, Mali, Mauritania na Niger.
Ufaransa imetuma wanajeshi wake katika eneo hilo kukabailiana na makundi ya kijihadi, wakati huu rais Macron akitangaza kupunguza kikosi kinachoshiriki kwenye operesheni inayoitwa, Barkhane.
Wiki kadhaa zilizopita, Mahamat alisema Chad itaendelea kuonesha uongozi katika mapambano dhidi ya makundi ya kijihadi, na imetuma wanajeshi wake nchini Mali inakoshirikiana na vikosi vya Ufaransa.
Mahamat ibn Idriss Déby Itno, anayefahamika kwa jina maarufu la Mahamat Kaka, ni Mwenyekiti wa Baraza la mpito la uongozi wa jeshi na rais wa mpito baada ya kifo cha baba yake Idriss Déby.
Idriss Deby, alifariki dunia mwezi Aprili, akiwa kwenye uwanja wa mapambano akiongoza jeshi la nchi yake dhidi ya wanajihadi Kaskazini mwa nchi hiyo.