Coronavirus: Zaidi ya kesi mpya 13,400 zathibitishwa nchini Ujerumani
Idadi ya kesi zilizothibitishwa za maambukizi ya virusi vya Corona nchini Ujerumani imepanda hadi 2,594,764, baada ya kesi mpya 13,435 kuthibitishwa siku moja iliyopita, kulingana na takwimu zilizotolewa na Taasisi ya magonjwa ya kuambukiza ya nchini Ujerumani Robert Koch (RKI).
Imechapishwa:
Taasisi hiyo pia imeripoti vifo vipya 249, na kufikisha jumla ya vifo 73,905 tangu kuzuka kwa janga hilo nchini Ujerumani.
Hayo yanajiri wakati mataifa kadhaa ya bara la Ulaya, yamesitisha kutoa chanjo ya AstraZeneca kuzuia maambukizi ya Covid-19 kwa watu wake, kwa hofu kuwa, chanjo hiyo inasababisha kuganda kwa damu mwilini.
Shirika la afya duniani WHO limekuwa likisema chanjo hiyo ni salama na inaendelee kutumiwa kwa sababu hakuna ushahidi mpaka sasa kuwa inasababisha madhara.
Hata hivyo, maafisa wa WHO walikutana siku ya Jumanne, kutathmini zaidi usalama wa chanjo hiyo ambapo mamilioni ya watu kote duniani, tayari wameshapata chanjo hiyo.