Tusk atoa wito kwa wahamiaji wa kiuchumi kusalia makwao
Rais wa Baraza la Ulaya Donald Tusk baada ya ziara yake nchini Ugiriki, anakutana kwa mazungumzo leo Ijumaa mjini Istanbul na Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan, siku tatu kabla ya mkutano muhimu na Uturuki juu ya mgogoro wa wahamiaji barani Ulaya.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kwa upande wake, Rais François Hollande anampokea Ijumaa hii asubuhi Kansela wa Ujerumani Angela Merkel katika Ikulu ya Elysée, katika kujaribu kupata suluhu kwa mgogoro unaowatia wasiwasi viongozi hao wa Ufaransa na Ujerumani.
Alhamisi Machi 3, Donald Tusk amewatolea wito wahamiaji wa kiuchumi kutothubutu kuingia barani Ulaya na kupania kuchukua hatua mpya kwa kupunguza kasi wimbi la wahamiaji ambao "bado ni wengi mno".
Wakati wa ziara yake nchini Ugiriki, kwenye mstari wa kwanza, Tusk alijaribu kukatisha tamaa wahamiaji wa kiuchumi. "Msije Ulaya. Msiwi na imani na wapitanjia. Msihatarishi maisha yenu na fedha. Yote hayo hayatosaidia chochote," Bw Tusk alisema mjini Athens.
"Ugiriki wala nchi yoyote ya Ulaya haiwezi kuendelea kuwa nchi inayowapa nafasi ya kupita wahamiaji," Tusk ameonya, huku akibaini kwamba "sheria za Schengen zitaangaliwa upya."
Jumatano wiki hii, nchini Slovenia, Tusk alibaini kwamba wanapania kurejelea sheria zihusuzo nchi zinazotumia viza ya Schengen, ikiwa ni pamoja na udhibiti mkali katika mipaka yake ya nje. Utaratibu huo ni moja ya suluhu ya mgogoro wa wahamiaji.