Barcelona Kumenyana na Real Madrid katika fainali ya Super Cup.
Nairobi – Na Paulo Nzioki
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kocha wa Barcelona Xavi Hernandez amekiri kwamba wapinzani wao wakuu katika ligi ya laliga, Real Madrid wako katika hali nzuri zaidi na wanaweza kuhifadhi Kombe la Super Cup la Uhispania.
Miamba hao wa Uhispania wanapambana katika fainali ya El Clasico hapo kesho huko Saudi Arabia katika uwanja wa Al –Awwal.
"Tutajaribu kutawala mchezo, kama ilivyo kawaida yetu ya kucheza na kuutawala uwanja. Tupo katika hali ya chini kidogo kuliko Real Madrid." alisema Xavi katika mkutano na wanahabari mjini Riyadh siku ya Jumamosi.
Mabingwa mara 14 wa Super Cup, Barcelona wako katika nafasi ya tatu kwenye La Liga, hivi majuzi wakipokea vipigo vya kushtukiza kutoka kwa Shakhtar Donetsk na Royal Antwerp kwenye ligi ya mabingwa, ingawa walifuzu kwa hatua ya mtoano ya kundi lao bila matatizo.
Kocha wa Real Madrid Carlo Ancelotti kwa upande wake amesema mlinzi Dani Carvajal atacheza licha ya kutofanya mazoezi na wachezaji wenzake siku ya Ijumaa.
Aidha Kocha Ancelotti alikataa kufichua ikiwa ni Kepa Arrizabalaga au Andriy Lunin atakayekua mlinda lango wa kikosi kitakachoanza mechi.
"Kwa sasa sijisikii kama naweza kuchagua mmoja kuwa wa kwanza na mwingine kuwa mbadala, na nadhani wote wawili wanaelewa hilo."
Ancelotti ana nafasi ya kumfikia Zinedine Zidane kama kocha wa pili mwenye mafanikio zaidi Madrid kuwahi kushinda katika fainali nyingi iwapo atashinda taji la 11 akiwa na vijana wa Los Blancos.
Fainali ya mwaka huu ni kama marudio ya pambano la mwaka jana ambapo Barcelona walifanya vyema na kushinda kombe la kwanza chini ya uongozi wa wa Xavi.
Mechi hio itachezwa hapo kesho saa nne usiku kwa saa za afrika mashariki.