Pata taarifa kuu
Tong-Il Moo-Do

Kenya yahifadhi ubingwa wa mashindano ya Tong-Il Moo-Do kwa mara ya 11

Mombasa, Kenya – Timu ya taifa ya Kenya mchezo wa Tong-Il Moo-Do, Jasiri imehifadhi taji la Mombasa Open kwa mara ya 11 katika mashindano yaliyokamilika siku ya Jumanne katika ukumbi wa Akademia ya Agha Khan jijini Mombasa nchini Kenya.

Wachezaji wa Kenya na mmoja wa Zambia kwenye sherehe ya kutuzwa baada ya mashindano ya Mombasa Open kukamilika mnamo 19/12/2023
Wachezaji wa Kenya na mmoja wa Zambia kwenye sherehe ya kutuzwa baada ya mashindano ya Mombasa Open kukamilika mnamo 19/12/2023 © Kenya Tong Il Moo Do Federation media
Matangazo ya kibiashara

Kenya ilishinda kwa jumla ya medali 191 ambayo ni medali 10 zaidi ya waliyopata katika mashindano ya mwaka jana. Kati ya 191 - 46 ni za dhahabu, 52 za fedha na 93 za shaba kwenye vitengo tofauti. 

Nahodha wa Jasiri Elvis Malupe akizungumza na Rfi Kiswahili Michezo, alionesha furaha yake huku akitoboa siri ya muendelezo wa ushindi wa taji hilo.

Sisi kama Jasiri tumeonesha ujasiri wetu tukatetea taji letu. Tulihakikisha tuna wachezaji katika kila kitengo na ni wachezaji ambao wamebobea kwenye mchezo huu.

Mchezaji wa Kenya wa Tong Il Moo Do kwenye hafla ya kuonyesha mbinu na sifa zake
Mchezaji wa Kenya wa Tong Il Moo Do kwenye hafla ya kuonyesha mbinu na sifa zake © Kenya Tong Il Moo Do Federation media

Rais wa shirikisho hilo nchini Kenya, Clarence Mwakio aliipongeza timu ya taifa kwa juhudi walizoonesha bila kusahau ufadhili wa dola elfu 646.4 waliopata kutoka kwa serikali kuu kupitia wizara ya michezo nchini Kenya chini ya waziri Ababu Namwamba.

Tulitarajia timu 42 lakini tukabahatika kupata 13, tukisonga mbele tunatarajia kuwa na mashindano mengi bora zaidi kuliko haya ambayo yataweza kukuza vipaji, mchezo huu hapa Kenya na Afrika kwa jumla.

Rais wa shirikisho la Tong Il Moo Do nchini Kenya na barani Afrika, Clarence Mwakio
Rais wa shirikisho la Tong Il Moo Do nchini Kenya na barani Afrika, Clarence Mwakio © Kenya Tong Il Moo Do Federation media

Aidha rais aligusia uwezekano wa kuandaa mashindano ya Mombasa Open mwezi Agosti kutoka mwezi Disemba kama ambavyo imekuwa kwa miaka iliyopita, kutokana na ukosefu wa ndege za usafiri kuingia Kenya wakati huu wa msimu wa utalii.

DRC ilimaliza nafasi ya tisa kwa medali moja tu, Zambia ikimaliza ya tatu kwa medali 23 (10 za dhahabu, 5 za fedha na 8 za shaba). Mataifa mengine ya Afrika, Nigeria ilishikilia nafasi ya saba kwa medali nne - mbili za dhahabu na mbili za shaba nayo Cote D'Ivoire ikivuta mkia bila medali yoyote.

Ufilipino ilikuwa ya tatu kwa medali 11.

Msimamo wa jedwali wa mashindano ya 2023
Msimamo wa jedwali wa mashindano ya 2023 © Kenya Tong Il Moo Do Federation media

'Yaliyopita si ndwele ...'

Nahodha Elvis Malipe tayari analenga kufanya vizuri zaidi katika mashindano ya dunia ya mwaka 2024 yatakayofanyika nchini Ufilipino.

Ushindi huu unatutambulisha kama watu wa kuogopewa. Timu zingine zijitayarishe kwa upinzani mkali sana. 

Kenya ilishiriki Mashidano ya Dunia ya Tong-Il Moo-Do mara ya mwisho mwaka 2019 nchini Korea Kusini na ikamaliza nafasi ya pili. 

Tunalenga kupeleka timu kubwa sana Ufilipino kwa vile timu ya Ufilipino ina upinzani mkuu, lazima tuende kama tumejipanga vilivyo kupabana.

Kwenye hotuba yake rais Clarence Mwakio, alitaja umuhimu na nia ya mataifa ya Afrika kuanzisha mpango wa ufadhili wa masomo ya wachezaji kama njia mojawapo kuu ya kukuza mchezo huo barani Afrika. 

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.