Robert Sanchez amesajiliwa na Chelsea kuwa mlinda lango wake mpya
Nairobi – Chelsea imekamilisha usajili wa mlinda mlango wa Uhispania Robert Sanchez kutoka kwa wapinzani wao katika ligi kuu nchini England Brighton kwa mkataba wa miaka saba.
Imechapishwa:
Sanchez, ambaye alipoteza nafasi yake kwa Jason Steele katika kipindi cha pili cha msimu uliopita, ametia saini mkataba wa miaka saba na wakali hao wa Stamford.
Chelsea wamemtafuta kwa ajili ya kutoa ushindani kwa Kepa Arrizabalaga kufuatia kuondoka kwa Edouard Mendy aliyejiunga na klabu ya Al-Ahli ya Saudi Arabia.
"Tunafuraha sana kumkaribisha Robert hapa Chelsea. Anaongeza kwa ubora zaidi kwenye kitengo chetu cha walinda mlango," wakurugenzi wa michezo wa Chelsea Paul Winstanley na Laurence Stewart wamesema.
Sanchez anakuwa mchezaji wa sita kusajiliwa na Chelsea majira ya kiangazi wakijiandaa kwa msimu mpya na meneja Pochettino.
‘Can’t wait to get started!’ 🤳 pic.twitter.com/5aDbDwRv1n
— Chelsea FC (@ChelseaFC) August 5, 2023
Mkataba huo unaripotiwa kuwa na thamani ya pauni milioni 25 (dola milioni 32) huku kipengele cha ziada cha mauzo kikiwamo.
Sanchez mwenye umri wa miaka 25, aliwahi kufanya kazi na kocha wa makipa wa Chelsea Ben Roberts alipokuwa Brighton. Roberts aliondoka kwenda Stamford Bridge mnamo Septemba 2022.
Meneja mpya wa Blues Pochettino anarekebisha kikosi chake kufuatia msimu mbaya zaidi wa klabu hiyo katika ligi kuu ya Uingereza kwa takriban miaka 30.
Chelsea pia wamehusishwa na uhamisho wa kiungo Moises Caicedo, huku Brighton wakitajwa kutafuta dau la pauni milioni 100.
Wanafungua kampeni yao mpya ya kusaka taji la ligi kwa msimu wa mwaka 2023-24 nyumbani dhidi ya Liverpool mnamo Agosti 13.