Shirikisho la Soka la Afrika Kusini Lalaani Vurugu Katika Michezo
NAIROBI – Na Paul Nzioki
Imechapishwa: Imehaririwa:
Shirikisho la Soka nchini Afrika Kusini (SAFA) limelaani "uhuni na ujambazi" katika Mechi ya mchujo ambapo maafisa wa polisi walilazimika kufyatua risasi mjini Pietermaritzburg.
Tatizo lilizuka katika mechi ya Chuo cha Orbit dhidi ya Umsinga United katika nusu-fainali ya mchujo ya ABC Motsepe Ijumaa.
Rais wa SAFA Danny Jordaan akizungumza na shirika la habari la SABC Sport amesema watatoa adhabu ambayo italingana na uhalifu uliofanyika.
"Kilichotokea hakiko sawa kabisa, ni cha kukataliwa na kulaaniwa," amesema. "Wahusika lazima wachukuliwe hatua kali’’.
Kwa mujibu wa Kanali wa kituo cha polisi KwaZulu-Natal, Robert Netshiunda, washukiwa watashtakiwa kwa kesi ya kujaribu kuua.
"Kulikuwa na watu wengi sana uwanjani, kwa hivyo sisi kuwapata washukiwa sio jambo rahisi, Uchunguzi unaendelea.
"Wazazi wametupa watoto wao, kwa hivyo wana wasiwasi. Hebu fikiria ikiwa kesho watasema 'mtoto wao amefariki, amepigwa risasi kwenye mechi ya mchujo ya mpira'," kocha wa Orbit Pogiso Makhoye amesema kwa uchungu.
Shirikisho la michezo barani Afrika, (CAF) pia hivi majuzi lilishutumu mfululizo wa matukio ya vurugu katika viwanja vya michezo barani Afrika.
Tukio la hivi punde linakuja kama pigo kwa Afrika Kusini katika azma yao ya kuandaa Kombe la Dunia la Wanawake 2027.