Morocco mabingwa wa taji la Billie Jean King
Na: Jason Sagini
Imechapishwa:
Morocco ndio washindi wa taji la mashindano ya tenisi ya Billie Jean King mwaka 2023 yaliyoandaliwa jijini Nairobi nchini Kenya katika uwanja wa Nairobi Club.
Morocco ilihitaji mechi ya tatu ya wachezaji wawili kila upande kuilaza Tunisia 2-1 kwenye fainali baada ya kila taifa kushinda mechi moja ya mchezaji mmoja kila upande awali.
Aya el Aouni na Malak El Allami walitumia muda wa saa moja na dakika 44 kuwashinda Hassen Ben Feryel na Chiraz Bechri seti 2-1 za 7-6, 3-6, 6-0.
“Nahisi mwenye furaha sana, hatukuanza vizuri mashindano ila nafurahi mwishowe tumetoboa kumaliza wa Kwanza kama timu,” alizungumza Malk el Allami.
Morocco sasa itaiwakilisha Afrika kwenye mashindano ya EURO-Africa mwaka ujao.
“Nahisi vizuri sana nilikua kwenye shinikizo dakika za mwisho. Tumecheza vizuri na tumepata ubingwa. Nampongeza Malak kwa ushirikiano mzuri,” alisema Aya El Auoni.
Tunisia, kupitia Chiraz Bechri ilishinda mechi moja kwa seti 2-0 za 6-4, 6-4 dhidi ya Yasmine Kabbaj.
Uganda ilishinda mechi mbili leo dhidi ya Ushelisheli na kuepuka kushuka daraja. Patience Athieno alimlaza Zenab Kante seti 2-0 za 6-0, 6-1 naye Winnie Birungi akamshinda Marie-May Isnard seti 2-0 za 6-2,6-1.
“Nimefurahi sana kwa namna tulivyomaliza mashindano. Sasa tutarudi nyumbani kuimarisha wachezaji wetu kwa kukuza vipaji,” alisema kocha wa Uganda, Edward Odokcen.
Ushelisheli imeshushwa daraja hadi la nne barani Afrika, Uganda imemaliza nafasi ya 11 nayo Burundi nafasi ya 10 baada ya kupoteza mechi 2-1 dhidi ya Namibia.
Kenya ilimaliza nafasi ya tatu baada ya kuishinda Zimbabwe mechi 2-1. Angella Okutoyi na Alicia Owegi waliwashinda Sasha Chimedza na Rufaro Magarira seti 2-0 za 7-6, 7-6 baada ya Cynthia Cheruto kupoteza 2-0 dhidi ya Rufaro Magarira.
Okutoyi alimshinda Sasha 6-3, 6-4 kwenye mechi ya kwanza.
Zimbabwe, Nigeria, Ghana, Mauritius, Botswana na Namibia zimechukua nafasi ya nne hadi tisa mtawalia.