Tennis: Burundi yapata ushindi muhimu kusonga mbele kutafuta taji la Billie Jean King
Na: Jason Sagini
Imechapishwa: Imehaririwa:
Burundi imeboresha nafasi yake kwenye kundi B ya kunyakua taji la Billie Jean King baada ya kuilaza Ushelisheli mechi tatu kwa bila. Mwamini Bitungwa alimshinda Zenab Kante seti 2-0 za 6-4, 6-0.
Hoziane Kitambala alimshinda Ashaelle Bastienne seti 2-0 za 6-0, 6-0 kisha kwenye mechi ya wachezaji wawili kila pande Bitungwa na Hoziane wakawashinda Marie-May Isnard na Zenab Kante seti 2-0 za 6-1, 6-2.
“Ushindi wa leo ni mkubwa na unamaanisha kitu kikubwa sana. Tunafurahia,” alisema nahodha wa Burundi, Hoziane Kitambala.
“Tuna imani kesho pia tutashinda dhidi ya Ghana. Tumeshazoea hivi viwanja,” alisema Mwamini Bitungwa.
Zaituni Akeza pia anaahidi ushindi kwa kujitahidi kwenye mechi ya mwisho akiwaomba mashabiki wa Burundi kujitokeza kuwashabikia mitandaoni.
Burundi sasa inashikilia nafasi ya tano kwa alama moja mbele ya Ushelisheli ambayo haijashinda mechi yoyote.
“Imekua siku ngumu lakini bado tuna nafasi sababu tunacheza na Kenya kesho. Ikiwa mbaya sana sidhani tutamaliza chini ya nafasi ya tatu, ” alisema kocha wa Nigeria Rotmi Akinloye.
“Tunajua Nigeria ni wapinzani wazuri, tunasubiri mechi kali na wasichana wangu wako tayari. Naomba mashabiki waje kwa wingi tushinde pamoja, ” alisisitiza kocha wa Kenya Francis Rogoi.
Kesho ni siku ya mwisho ya hatua ya makundi kabla ya hatua ya mtoano siku ya Jumamosi.