Tennis: Burundi yapata ushindi wa kwanza, mashindano ya Billie Jean King
Na: Jason Sagini
Imechapishwa: Imehaririwa:
Baada ya kupoteza mechi zote tatu siku ya kwanza, Burundi imepata ushindi wao wa kwanza leo dhidi ya Zimbabwe ambapo Hoziane Kitambala alimshinda Rufaro Magarira seti 2-0 za 6-3 na 7-5.
Awali kwenye mechi ya kwanza, Akeza Zaituni alipoteza seti 2-0 dhidi ya Sasha Chimedza, alama sawa na kwenye mechi ya doubles ambapo Hoziane Kitambala na Zaituni Akeza walishirikiana dhidi ya Eunice Mauchi na Tanyaradzwa Midzi.
“Mechi ilikua nzuri, mpinzani wangu nilikuwa namfahamu vizuri. amesema Hoziane ambaye pia ndiye nahodha wa Burundi.
“Tunatarajia kufanya vema katika mechi zijazo,” ameongeza Hoziane.
Kwa siku ya pili mfululizo, Uganda imepoteza mechi zake zote dhidi ya Morocco na kusalia chini ya jedwali kwenye kundi A.
Abigail Nabasinga alipoteza seti 2-0 za 6-0, 6-1 dhidi ya Manal Ennaciri naye Winnie Birungi akapoteza seti 2-0 za 6-1, 6-0 dhidi ya Yasmin Kabajj. Edinah Nabiryo na Patience Athieno walipoteza seti 2-0 za 6-0, 6-0 dhidi ya Malak El Allami na Aya El Aouni kwenye mechi ya doubles.
Kocha wa Uganda Edward Odokcen bado ni mwenye imani kubwa licha ya Uganda kupoteza mechi zote.
“Idadi kubwa ya wachezaji wetu ni wageni, lakini pia nchi yetu haina mpango wa kuendeleza mchezo huu," amesema Odoksen.
Kenya ilionesha ubabe kwa kuishinda Botswana mechi zote tatu. Alicia Owegi alimshinda Cheludo Monayoo seti 2-1 naye Angella Okutoyi akamshinda Chelsea Chakanyuka 2-0 kisha kwenye doubles pacha Okutoyi na Roselida Asumwa wakawashinda Chelsea na Kelebogile Monnayoo seti 2-0.
Nigeria ingali kileleni mwa kundi A ikifuatiwa na Kenya. Tunisia na Zimbabwe zinaongoza kundi B huku Burundi ikipanda hadi nafasi ya tano.