Mbappe hataongeza mkataba wake na PSG
NAIROBI – Klabu ya Paris St-Germain ya nchini Ufaransa huenda ikaamua kumuuza mchezaje wake Kylian Mbappe msimu huu wa joto badala ya hatari ya kumpoteza bila malipo katika muda wa mwaka mmoja, hatua hii ikija baada ya mchezaji huyo kuiambia klabu hiyo kuwa hataongeza mkataba wake.
Imechapishwa:
Mkataba wake wa sasa unamalizika mwishoni mwa msimu ujao akiwa na chaguo la kuongeza mwaka mwingine katika klabu hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa, kulikuwepo na makataa ya Julai 31 kwa Mbappe, 24, kuiambia PSG iwapo alikuwa anawazia kufanya mkataba wake upya hadi mwaka wa 2025.
Baada ya mazungumzo ya miezi kadhaa, mchezaji huyo ameitumia klabu hiyo barua akisema hatofanya hivyo.
Mfungaji huyo bora wa PSG atakuwa huru kuondoka bila malipo mwishoni mwa msimu ujao na hatua hiyo inaweza kuwa mbinu ya kufanya mazungumzo.
Hata hivyo, wakati mabingwa hao wa Ufaransa wakijaribu kurekebisha sera ya michezo kwa timu yao baada ya miaka mingi ya kununua wachezaji nyota bila mkakati madhubuti, PSG wameazimia kutomwacha Mbappe kwenda bure, huku klabu hiyo ikikerwa na barua ya mchezaji huyo iliyovujishwa kwenye vyombo vya habari kwanza kabla ya wao kuiona.
Ina maana kwamba wasipopata hakikisho kuhusu nia ya baadaye ya mshindi huyo wa Kombe la Dunia 2018, watamuuza katika hatua ambayo itaweka vilabu vinavyoongoza barani Ulaya kuwa macho.
Real Madrid wamekuwa wakitaka huduma za Mfaransa huyo kwa muda mrefu na alikataa kuhamia Bernabeu kusalia PSG mwaka jana.
Kuondoka kwa Karim Benzema kuelekea nchini Saudi Arabia kunamaanisha kuwa Real inahitaji mshambuliaji, ingawa inamwazia mchezaji wa Tottenham kuwa Harry Kane.
Mbappe, ambaye alijiunga na PSG mwaka 2017 kwa mkopo akitokea Monaco kabla ya uhamisho wa euro 180m na amefunga mabao 212 katika michezo 260.
Ana mabao 38 katika mechi 68 alizoichezea Ufaransa, ikiwa ni pamoja na mabao matatu kwa mpigo katika fainali ya mwaka jana nchini Qatar, Ufaransa iliposhindwa na Argentina kwa mikwaju ya penalti.
Mbappe alimaliza kama mfungaji bora wa Ligue 1 katika kila misimu mitano iliyopita na ameshinda mataji matano ya ligi katika misimu yake sita akiwa PSG.
PSG ilimaliza msimu wa 2022-23 kwa kutwaa taji la Ligue 1 pekee baada ya kushindwa tena kutwaa taji la Ligi ya Mabingwa, na kufungwa na Bayern Munich katika hatua ya 16 bora.
Mbappe atakuwa mshambuliaji wa pili mwenye hadhi ya juu kuondoka Parc des Princes msimu huu, baada ya mshambuliaji wa Argentina Lionel Messi kuondoka mwishoni mwa kandarasi yake ya miaka miwili na kujiunga na Inter Miami ya Ligi Kuu ya Soka.