Tennis: Kenya yaanza vema mashindano ya Billie Jean King Cup
Na: Jason Sagini
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kenya imeanza vizuri kwenye mashindano ya Billie Jean King Cup ya mwaka huu kwa kushinda mechi mbili dhidi ya Morocco katika uwanja wa Nairobi Club nchini Kenya.
Angella Okutoyi alishinda seti 2-0 dhidi ya Mallack El Ellami na kuvuna ushindi mwingine wa seti 2-0 katika kitengo cha doubles aliposhirikiana na Cynthia Cheruto.
Morocco ilipata ushindi mmoja dhidi ya Kenya wakati Aya el Aouni alimlaza Alicia Owegi seti 2-0. Kenya inaorodheshwa nafasi ya kumi na moja nayo Morocco nafasi ya kwanza barani Afrika.
“Kuishinda Morocco ni kitu cha kujivunia na imetupa motisha zaidi ya kufanya vizuri kwenye mashindano, “ amesema kocha Francis Rogoi.
“Sikuwa naangalia nacheza na nani, nilizingatia tu jinsi ya kudhibiti mchezo na hio ilinisaidia sana kukusanya alama za kutosha, “ amesema Angella Okutoyi.
Great fighting spirit from @frmtennis . Truly a worthy opponent ✨#BillieJeanKingCupKe pic.twitter.com/Kq1AaKkdVW
— Tennis Kenya (@tennis_kenya) June 12, 2023
Aidha haikua siku nzuri kwa wachezaji wa Burundi na Uganda kwani walipoteza mechi zote tatu dhidi ya Mauritius na Nigeria mtawalia.
“Leo Nigeria wametushinda mechi zote kwa sababu hivi viwanja ni vipya hatujavizoea lakini nina imani kesho tutacheza vizuri, “ alisema kwa kusikitika mchezaji wa Uganda Winnie Birungi.
Kauli hii pia aliunga mkono mchezaji wa Burundi Bitungwa Mwamini.
Baada ya siku ya kwanza, Tunisia na Nigeria zinaongoza kwenye makundi. Kenya inashikilia nafasi ya pili kwenye kundi A wakati Burundi na Uganda zinavuta mkia kwenye makundi yao.