Senegal ndio mabingwa wa AFCON chini ya wachezaji wasiozidi umri wa miaka 17
NAIROBI – Taifa la Senegal limeendelea kudhibitisha ubabe wao wa soka baada ya kushinda taji la AFCON kwa wachezaji wa kiume wasiozidi umri wa miaka 17.
Imechapishwa:
Katika fainali iliyochezwa hapo jana usiku, Senegal walifanikiwa kupata ushindi baada ya kutoka nyuma na kuishinda Morocco mabao 2-1 katika fainali iliyochezwa kwenye uwanja wa Nelson Mandela, Algiers.
Mamadou Sawane aliyetokea benchi kipindi cha pili alifunga kwa kichwa bao la ushindi dakika saba kabla ya mechi kumalizika huku Senegal wakifunga mabao mawili ndani ya dakika nne na kubadilisha bao la mapema la nahodha wa Morocco Abdelhamid Ait Boudlal na kuleta faraja kwa simba hao wadogo wa Teranga.
Serigne Falou Diouf alikuwa ameisawazishia Teranga Cubs katika dakika ya 79 kufuatia penalti iliyotolewa na VAR.
Senegal sasa imeshinda mataji matatu ndani ya miezi minne, timu yao ya wachezaji wa ndani wakiwa wameshinda taji la Ubingwa wa Mataifa ya Afrika (CHAN) mwezi Februari huku pia wakishinda taji la U20 AFCON nchini Misri mwezi Machi.
Timu yao ya taifa ya wakubwa, Simba ya Teranga ilianza kutawala bara mwaka jana iliponyanyua taji la AFCON 2021 baada ya kuwalaza wenyeji Misri na kisha kuendelea na taji la AFCON katika soka ya ufukweni baadaye mwakani.
Wawakilishi wa Afrika Mashariki katika michuano hii Somalia walishindwa kufuzu kuingia hatua ya mtoano baada ya kumaliza katika nafasi ya mwisho ndani ya kundi C.
Sudan Kusini waliondolewa baada ya kuibuka kwa madai ya udanganyifu wa umri.