Barcelona ina nia ya kumrejesha Messi Camp Nou
NAIROBI – Rais wa timu ya kandanda ya Barcelona Joan Laporta amesema kuwa timu hiyo itafanya kila juhudi kihakikisha kuwa nyota wa taifa la Argentina Lionel Messi amerejea katika timu hiyo inayoshiriki ligi kuu ya kandanda nchini Uhispania.
Imechapishwa:
Mshambuliaji huyo wa timu ya Paris Saint-Germain ya Ufaransa anatarajiwa kuondoka katika timu hiyo mwishoni mwa msimu huu baada ya kandarasi yake kukamilika na mabingwa wapya wa La Liga Barcelona wanatarajiwa kumshawishi ajiunge nao licha ya timu ya Al Hilal ya Saudi Arabia kusaka sajili yake.
Messi hajakuwa na msimu mzuri tangu ajiunge na PSG kutokea Barcelona aliposhinda mataji manne ya klabu bingwa barani ulaya, mataji 10 ya ligi kuu nchini Uhispania La Liga na vile vile kupata ufuasi mkubwa katika timu hiyo ya Uhispania.
Laporta amesema kuwa amezungumza na Messi na kujaribu kutengeneza uhusiano kati yake na timu hiyo ambao uliharibiwa mwaka 2021 alipokuwa akiondoka Barcelona.
Messi alikuwa anataka kusalia Barcelona lakini timu hiyo haingeweza kumudu kumlipa kutokana na deni la zaidi ya euro bilioni moja (dola bilioni 1.1).
"Nimezungumza na Leo kwa namna fulani na kumwelezea hali ambayo ilitokea, ilibidi niweke klabu mbele ya kila kitu, hata yeye, ambaye ni mchezaji bora zaidi duniani," Laporta alisema haya katika runinga ya taifa mjini Catalan TV3.
"Ukweli ni kwamba yalikuwa mazungumzo ya upendo, mazungumzo mazuri zana, na pia nimekuwa nikimtumia ujumbe- hivi majuzi nilimpongeza kwa kushinda Kombe la Dunia."
Kutokana na ushindi wa Barcelona wa 4-2 dhidi ya Espanyol, ushindi uliowapa taji la La Liga msimu huu, Laporta aliandika katika mtandao Twitch na kusema, "tutafanya kila liwezekanalo" kumsajili Messi."
Lakini, akizungumza kwenye tuninga ya TV3, alikuwa makini zaidi.
"Yeye ni mchezaji wa Paris Saint-Germain na kile ambacho tutakachokifanya ni kuimarisha kila sehemu katika timu, na tayari tumefanya hivyo," alisema Laporta.
"Nadhani nitafanya vibaya kuzungumza kuhusu maswala haya kuhusu Leo, kwa sababu yeye ni mchezaji wa timu ya Paris Saint-Germain,na lazima tusubiri hadi mwisho wa msimu ndio tufanye mazungumzo haya bila wasiwasi."
AFP iliripoti wiki iliyopita kwamba duru za kuaminika zimedhibitisha kuwa ni "mkataba uliokamilika" kwamba Messi atahamia Saudi Arabia msimu ujao.
Lakini, Laporta amesema licha ya pesa zinazotolewa na timu ya Saudi Arabia zinazoripotiwa kuwa dola milioni 400 kwa mwaka, Barcelona inaweza kushindania kupata saini ya Messi.
"Kwa heshima zote kwa Saudi Arabia, Barca ni Barca, na ni nyumbani kwake," aliongeza Laporta.
"Tunaweza kushindana na kila mtu. Historia inatuunga mkono, hisia ni kali sana, tuna mashabiki milioni 400 kote duniani."
Barcelona inahitaji kuaanda zaidi ya euro milioni 200 katika akiba yake, au mapato mapya, ili kuweza kuendesha oparasheni zake za kazi bila vikwazo chini ya sheria za wachezaji wa La Liga.