Super Eagles wanahitaji utulivu kurejelea ubora wao: Jay Jay Okocha
NAIROBI – Na Paul Nzioki
Imechapishwa: Imehaririwa:
Nahodha wa zamani wa timu ya taifa ya soka kwa wanaume nchini Nigeria, Super Eagles, Austin Jay Jay Okocha, amewataka wachezaji wa timu ya taifa kuwa na msimamo na utulivu zaidi katika harakati zao za kudumisha hadhi na ubabe wa timu hiyo barani Afrika.
Kiungo mkabaji huyo wa zamani alitoa ushauri huo katika mahojiano na Shirika la Habari la Nigeria (NAN) wakati wa uzinduzi wa mashindano ya “Penalty Cup African Heroes” mjini Lagos hapo Alhamisi ya wiki hii.
Okocha, ambaye ndio kwanza amesherehekea miaka 30 ya mwito wake wa kwanza kwenye timu ya taifa ya wazee, alisema timu ya Super Eagles imeonekana kupoteza umaarufu wake katika miaka ya hivi majuzi baada ya Kukosa mashindano muhimu kama Kombe la Dunia.
“Sote tunataka kuwaona Super Eagles wakifanya vizuri, tunajua jinsi inavyoumiza kutokuwa kwenye Kombe la Dunia, timu inahitaji kusawazisha.” Alisema Okocha.
"Super Eagles wanahitaji kuwa thabiti zaidi, jambo ambalo ni dhahiri sana kwamba sivyo. Sote tunajua kuwa sisi ni taifa linalojidai sana linapokuja suala la soka.” Aliongeza kusema Okocha.
Aidha kuhusu suala la vipaji, gwiji huyo alisema kuwa Nigeria sio kwamba haina vipaji na kinachohitajika tu ni kuweka timu imara na kuleta umoja na katika hali ambayo inaweza kuwakilisha taifa jinsi inavyopaswa.
"Sisi kama wachezaji wa zamani tutawaunga mkono na kuwatakia kila la heri," alisema.
Kuhusu kuongezwa kwa mkataba wa kocha wa sasa wa Super Eagles, Jose Pesseiro, Okocha ameeleza kuwa alitarajia Shirikisho la Soka la Nigeria Kuchukua uamuzi sahihi.
“Mpira wa miguu ni mchezo unaotegemea matokeo, timu ikifanya vizuri inapata sifa na isipokua inafanya vizuri inakua vinginevyo. Kocha asipofanya vizuri, uteuzi wake utakuwa mashakani. Alielezea Jay Jay Okocha.
Kuhusu suala hilo la kocha wa timu ya taifa, Okocha alisema kuwa katika nafasi yake angeshauri NFF nini cha kufanya kuhusu kandarasi ya Pesseiro, kwa sababu wanapaswa kuchukua uamuzi wa busara na kuurekebisha Pia ikibidi.
Okocha pia alimshauri mshambuliaji wa Nigeria aliye katika ubora wake kwa sasa, Victor Osimhen kujiamini na kutumia nafasi inayopatikana kwake.
Mchezaji huyo wa zamani wa Paris Saint German pia alisema kushiriki kwake katika michuano ijayo ya “African Heroes Penalty Cup” kutampa nafasi ya kuungana tena na wachezaji wenzake wa zamani katika soka.
NAN inaripoti kuwa Okocha ndiye aliyewezesha kuwepo kwa mashindano hayo, ambapo atashiriki pamoja na Daniel Amokachi na Finidi George kuiwakilisha Nigeria.
Michuano ya “African Heroes Penalty Cup” itafanyika Lagos katika tarehe ambayo bado haijatangazwa baadae mwakani.
Nchi nane za Afrika ambazo zitashiriki katika toleo la uzinduzi ni pamoja na Nigeria kama mwenyeji, Morocco, Ghana, Afrika Kusini, Cameroon, Mali, Cote D'Ivoire na Senegal.
Kila nchi itakuwa na wawakilishi watatu kucheza mchezo wa robo fainali ya mtoano hadi washiriki kwa fainali na kutoa Mshindi wa shindano hilo.