Napoli wameshinda taji la kwanza la Serie A baada ya miaka 33.
NAIROBI – Na Paul Nzioki
Imechapishwa:
Napoli wameshinda taji lao la kwanza la ligi kuu nchini Italia maarufu Scudetto tangu 1990 baada ya bao lake Victor Osimhen katika kipindi cha pili na kupata sare ya 1-1 dhidi ya Udinese Alhamisi usiku.
Hii ni baada ya jumapili iliyopita klabu ya Salernitana, kuaribu sherehe zao walizopanga kwa kulazimisha sare.
Napoli sasa wamerekebisha makosa yao na kuweka pengo la alama 16 huku ikiwa imesalia mechi tano pekee msimu kumalizika.
Mshambuliaji Victor Osimhen raia wa Nigeria hajakosa kuonyesha mashabiki wa Napoli furaha aliokua nayo baada ya kupata ushindi huo.
"Nina furaha kwa mashabiki wote wa Napoli duniani kote," Osimhen alisema. "Hakuna anayestahili Scudetto zaidi ya Neapolitans - zaidi yetu. Sikujali nani atafunga, nilitaka tu kupata Scudetto."
"Nataka kufurahia wakati huu kwa maisha yangu yote. Kisha baada ya msimu ndoto zangu zingine zinaweza kuja,” Osimhen aliendelea. "Lakini kwa sasa sio wakati wa kuzungumza juu ya ndoto zangu zingine. Nilitaka kushinda hii."
"Napoli, hii ni kwa ajili yako," kocha Luciano Spalletti alisema. "Kuna watu hapa ambao wataweza kupitia nyakati ngumu katika maisha yao kwa sababu wanakumbuka wakati huu. Watu hawa wanastahili furaha yote.”
Ni mara ya kwanza kwa klabu Kutoka kusini mwa miji mikuu ya soka ya Italia ya Milan na Turin kushinda ligi tangu Roma ilipotwaa taji hilo mwaka wa 2001.
Zaidi ya wafuasi 50,000 walikusanyika kwenye Uwanja wa Diego Armando Maradona huko Naples, ambapo mechi hiyo ilionyeshwa kwenye skrini kubwa.
Mashabiki hao, pai nao wametangaza furaha yao. Kevin, mfuasi ambaye alikataa kutaja jina lake la ukoo, akizungumza na kituo kimoja cha Runinga uko Italia ambapo alisema sherehe itakua kubwa kwa ajili ya Scudetto.
"Kila mara mliniambia, 'Tunataka kushinda,' na sasa tumeshinda. Tumeshinda sote pamoja,” Rais wa Napoli Aurelio De Laurentiis aliambia mashabiki kabla ya kumkumbatia Meya wa Naples Gaetano Manfredi.
De Laurentiis alichukua klabu hiyo mwaka 2004 baada ya Napoli kutangazwa kuwa imefilisika, na kuanza tena ligi daraja la tatu.
"Huku ni kutawazwa kwa ndoto ambayo imekuwa ikiendelea kwa miaka 33," De Laurentiis aliongeza akisema kuwa mchakato huo umechukuwa muda mrefu.
Ubalozi wa Marekani nchini Italia ulitoa tahadhari ya usalama wiki iliyopita kwa raia wake, ukisema "sherehe za kawaida zinaweza kudumu siku nyingi" na kuonya kufungwa kwa barabara wakati wa sherehe za wafuasi wa Napoli.
Napoli wameongoza jedwali kwa muda mrefu wa msimu, wakionyesha soka bora na la kufurahisha zaidi, wakiongozwa na Osimhen na winga wa Georgia Khvicha Kvaratskhelia. Wamepoteza mechi tatu za ligi msimu mzima.
Pia walionyesha nia ya kupiga hatua kwenye ligi ya mabingwa barani Ulaya kabla ya kushindwa kwa jumla ya mabao 2-1 dhidi ya Milan katika hatua ya robo fainali.