Kenya: AFC Leopards (Ingwe) kupinga maamuzi ya shirikisho
NAIROBI – Na Mchambuzi wetu Paul Nzioki
Imechapishwa: Imehaririwa:
Klabu ya soka nchini kenya, AFC Leopards imeamua kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa shirikisho la kandanda nchini humo FKF, kuwapa adhabu kali kufuatia fujo zilizotokea Jumapili wakicheza na Kakamega Homeboyz ugani Bukhungu,Magahribi ya taifa hilo la Afrika Mashariki.
Akidhibitisha taarifa hio Kwenye mahojiano ya simu, Katibu mkuu wa klabu ya Afc Leopards Bwana Gilbert Andugu, amesema hawawezi kuvumilia dhulma kama hizo.
Bwana Andugu ameilaimu kamati iliyofanya maamuzi hayo, kwa kufanya maamuzi pasipo na uchunguzi wa kina kuhusu sababu za fujo hizo na waliohusika.
‘’Tutaelekea Mahakamani kukata rufaa dhidi ya uamuzi wao. Uamuzi huo unaonyesha wazi kuegemea upande mmoja. Baadaye tutatoa taarifa kama klabu kwa mashabiki wetu kuwaelekeza,’’ amesema Andugu.
Leopards maarufu kama Ingwe, imepigwa faini ya shillingi laki tano pesa ya Kenya, kucheza mechi nne zifuatazo za nyumbani bila mashabiki na kugharamia malipo ya matibabu ya mwamuzi Michael Obuya aliyeumia wakati wa fujo hizo.
Katika barua iliyotiwa saini na afisa mkuu wa shirikisho la mpira nchini Kenya FKF, Barry Otieno, Homeboyz waliokuwa wakiongoza kutokana na bao la Hillary Otieno wamepewa ushindi wa mechi hiyo iliyotibuka katika dakika ya 34 kutokana na fujo za mashabiki.
Barua hiyo vile vile imependekeza kocha mkuu, Patrick Aussems na mkufunzi wa mkipa Lawrence Webo wachukuliwe hatua za kinidhamu kuwajibikia vitendo vyao wakati wa mechi hiyo.
FKF imesema ripoti kuhusu mechi imewalaumu mashabiki wa Leopards waliolalamika kuhusu uamuzi refari wa mechi hiyo baada ya kipa Farouk Shikalo kuuzuia mpira akiwa nje ya eneo la hatari.
Ripoti imesema mashabiki wa Leopards walitaka kipa huyo apewe kadi nyekundu kwa kosa hilo, lakini mwamuzi alikataa kumuadhibu.
Baada ya taarifa hiyo kutolewa mwenyekiti wa klabu hiyo, Dan Shikanda aliwatetea vikali mashabiki wa klabu yake, huku akidai mwamuzi ndiye aliyesababisha fujo hizo kwa kutofuata sharia za Fifa.
Shikanda pia alidai, Leopards ni timu kubwa na lazima usalama wa kutosha uakikishwe wakati wa mechi zao.