Mbappe kuchukua majukumu ya unahodha wa timu ya taifa ya Ufaransa
NAIROBI – Kylian Mbappe atachukua unahodha wa timu ya taifa ya Ufaransa baada ya Hugo Lloris kustaafu soka la kimataifa.
Imechapishwa:
Baada ya timu yake kushindwa kwenye fainali ya Kombe la dunia dhidi ya Argentina, Lloris aliyekuwa nahodha kwa zaidi ya mwongo mmoja, aliamua kutungika dalugha.
Mshambuliaji wa Paris Saint-Germain Mbappe, 24, amekubali jukumu hilo baada yake kufanya mazungumzo na kocha Didier Deschamps.
Mbappe anatarajiwa kuanza majukumu yake ya kwanza kama naodha siku ya Ijumaa katika mechi za kufuzu kwa Euro 2024 dhidi ya Uholanzi kwenye Uwanja wa Stade de France, mechi ya kwanza kwa Les Bleus tangu fainali ya Kombe la Dunia huko Doha mnamo Desemba 18.
Mshambuliaji wa Atletico Madrid Antoine Griezmann atakuwa naibu wake baada ya beki wa kati wa Manchester United Raphael Varane naye pia kutangaza kustaafu soka la kimataifa.
Nahodha huyo mpya wa Ufaransa aliisaidia Les Bleus kutwaa ubingwa wa Kombe la Dunia mwaka wa 2018 nchini Urusi.
Tangu alipoanza kuichezea Ufaransa mwaka 2017, Mbappe mwenye umri wa miaka 24, ameichezea timu yake ya taifa mara 66 na kuifungia mabao 36.