Arsenal yapaa hadi nafasi ya 3, Tottenham yakwea nafasi ya 4
Goli la mtindo wa Nge, lililofungwa na mshambuliaji wa klabu ya Arsenal ya Uingereza, Olivier Giroud, lilitosha kuamsha chachu ya ushindi wa timu hiyo, ulioifanya timu hiyo kuchupa hadi katika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi.
Imechapishwa:
Pasi ya nyuma iliyopigwa na Alexis Sanchez, ilitosha kumpa nafasi mfaransa huyo, kuufikia mpira kwa mtindo wa aina yake na kufunga bao kwa mguu wa kushoto mpira ukitokea nyuma na kugongwa mwamba wa juu wa goli kabla ya kuingia nyavuni.
Bao la pili lililofungwa kwa kichwa na Alex Iwobi, lilitosha kuonesha wazi jahazi la klabu ya Crystal Palace linazama.
Ushindi huu wa Arsenal, unawavusha hadi katika nafasi ya tatu, alama 9 pekee zikiwa zimesalia nyumba ya vinara wa ligi hiyo, Chelsea, huku Palace wenyewe wakisalia kwenye nafasi ya 17, alama mbili pekee na timu zinazoshikilia mkia.
Palace wameshinda mchezo mmoja tu katika michezo 13 ya ligi, huku kocha Sam Allardyce akisubiri kupata ushindi wake wa kwanza toka alipochukua mikoba hiyo kutoka kwa Alan Pardew.
Katika mchezo mwingine,Watford walikubali kipigo cha mabao 4-1 kutoka kwa Tottenham ambao wamechupa hadi kwenye nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi hiyo.