Kenya na Tanzania zashindwa vibaya mechi ya kufuzu soka la ufukweni
Timu za taifa za soka za Kenya na Tanzania zina kazi kubwa mbele yao kufuzu katika fainali ya mataifa bingwa barani Afrika katika mchezo wa soka wa ufukweni utakaofanyika mwezi Desemba nchini Nigeria baada kupoteza mechi za nyumbani mwishoni mwa wiki iliyopita.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kikosi cha Kenya kikicheza mjini Mombasa, kilipata pigo baada ya kufungwa na Ghana mabao 10-3.
Matokeo hayo yalizua aibu kwa mashabiki wa Kenya waliokuja kwa wingi kujionea mchuano huo na kurejea nyumbani wakiwa vichwa chini baada ya aibu ya kufungwa.
Rais wa Shirikisho la soka nchini humo FKF Nick Mwendwa, amesema hakutarajia vijana wake kufanya vizuri kwa sababu bado kuna kazi kubwa ya kuuinua mchezo huo.
Mwendwa amesema Kenya itakuwa vizuri baada ya miaka minne na safari ya mwaka huu kwenda nchini Nigeria haiwezekani kamwe hasa baada ya kufungwa mabao 10 nyumbani.
Nchini Tanzania, hali ilikuwa kama hiyo baada ya kikosi hicho kufungwa mabao 7-3 katika mechi iliyochezwa katika uwanja wa Karume jijini Dar es salaam.
Kilichowashangaza wengi ni kwamba, mchanga kutoka baharini ulibebwa na kumwangwa kwenye uwanja wa nyasi bandia.
Mechi za marudiano zitapigwa katikati ya mwezi Septemba ugenini.
Mataifa manne wakiwemo wenyeji Nigeria yameshafuzu pamoja na Morocco, Libya na Misri.
Michuano hii ilifanyika mara ya kwanza mwaka 2006 nchini Afrika Kusini na Cameroon kuibuka mabingwa.
Senegal inaendelea kushikilia rekodi ya kushinda mataji mengi, hadi sasa imeshinda mara tatu mwaka 2008, 2011 na 2013.
Nigeria imeshinda mara 2 mwaka 2007 na 2009.
Madagascar ndio mabingwa mtetezi wa taji hili.