Rwanda yakwenda Brazil kusaka medali ya kwanza
Rwanda itawakilishwa na wanamichezo saba katika michezo ya Olimpiki inayofungua milango yake siku ya Ijumaa nchini Brazil.
Imechapishwa:
Wanamichezo hao watashiriki katika riadha, uongeleaji na kukimbiza baiskeli.
Ambroise Uwiragyie atashiriki katika mbio za Marathon kwa upande wa wanaume, huku Claudette Mukasakidi akishiriki katika mbio hizi kwa upande wanawake.
Mchezaji mwingine anayeshiriki katika riadha ni Salome Nyarirukundo ambaye atashiriki katika mbio za Mita 10000 kwa upande wa wanawake.
Adrien Niyonshuti na Nathan Byukusenge nao watashiriki katika mashindano ya kukimbiza baiskeli.
Upande wa wanaume Mita 50 mtindo wa Freestyle atakuwa ni Eloi Imaniraguha katika mchezo wa uogeleaji lakini Joannah Umurungi atashiriki katika uogeleaji Mita 100 mtindo wa Butterfly kwa upande wa wanawake.
Rwanda inakwenda katika michezo hii na matumaini ya kushinda medali ya kwanza, baada ya kushiriki katika michezo hii mara 8 mwaka 1984,1988,1992,1996,2000,2004,2008 na 2012.
Hata hivyo, Jean de Dieu Nkundabera aliishindia nchi yake medali ya shaba katika mbio za kukimbiza baiskeli kwa walemavu wakati wa michezo ya Olimpiki ya walemavu nchini Ugiriki mwaka 2004.
Nchi hiyo ya Afrika ya Kati haijawahi kushiriki katika michezo ya kipindi cha baridi.