Wanariadha wa Kenya wachuana katika mchujo wa kitaifa kufuzu michezo ya Olimpiki
Mamia ya wanariadha nchini Kenya, wanashiriki katika mchujo wa kitaifa kutafuta kikosi cha wanaraidha watakaowakilisha nchi hiyo katika michezo ya Olimpiki mwezi Agosti nchini Brazil.
Imechapishwa:
Mchujo huu kwa mara ya kwanza unafanyika mjini Eldoret leo na kesho katika uwanja wa Kipchoge Keino.
Mshindi wa kwanza na wa pili katika kila mbio atafuzu moja kwa moja katika michezo hiyo huku mshindi wa tatu akiamuliwa na makocha wa riadha.
Shirikisho la riadha nchini humo AK linasema zoezi hilo litakuwa wazi na matokeo yatakuwa haki kwa mwanariadha wote wanaoshiriki na watakaoshinda ndio watakaopewa nafasi hiyo.
Jackson Tuwei rais wa Shirikisho hilo amesema mchujo huu utasaidia Kenya kupata medali nyingi katika michezo hiyo.
Mchujo huu pia unawashirikisha wanariadha kutoka nchi jirani kama Uganda, Tanzania na Sudan ambao pia wanatafuta nafasi ya kuziwakilisha nchi zao nchini Brazil.
Miongoni mwa mbio zinazoshindaniwa ni pamoja na Mita 800, 1,500 3,000 5,000 10,000, 400 miongoni mwa nyingine.
Mbali na riadha, Kenya itashiriki katika mchezo wa raga kwa wachezaji saba kila upande, Tae kwo ndo, masumbwi na kunyanyua uzani.