Ufaransa, Uswisi zasonga mbele, Albania kusubiri hatma yake
Michuano ya kombe la Ulaya 2016, imeendela kushika kasi nchini Ufaransa, huku wenyeji wa michuano ya mwaka huu, Ufaransa wakifanikiwa kuongoza kundi A na kutinga hatua ya 16 bora.
Imechapishwa:
Ufaransa hapo jana usikuj ilicheza na Uswis kwenye mchezo ambao ulishuhudia timu hizi zikitoshana nguvu ya bila kufungana, sare ambayo unaofanya Uswis na Ufaransa kutinga hatua ya 16 bora huku Ufaransa ikiwa kinara wa kundi lake.
Mchezaji kiungo mshambuliaji wa Ufaransa, Paul Pogba, ambaye alifanyiwa mabadiliko zaidi ya mara tano kwenye mechi zilizopita za Ufaransa, jana alikuwa mwiba baada ya mashuti yake ya kwenye kipindi cha kwanza kugonga mwamba zaidi ya mara mbili.
Mshambuliaji aliyeingia kipindi cha pili, na ambaye katika mechi zilizopita aliifungia magoli timu yake, Dimitri Payet, nae alikosa mabao kadhaa baada ya mipira aliyoipiga kugonga mwamba wa juu.
Kwenye mchezo huo, Uswis almanusura wapate penati katika dakika za lala salama, wakati beki Bacary Sagna alipomvuta jezi Blerim Dzemaili, lakini mwamuzi hakutoa adhabuj hiyo.
Ufaransa sasa huenda ikacheza na mshindi wa tatu kutoka kwenye kundi C, D au E, hii ikiwa na maana kuwa huenda ikacheza na kati ya timu ya taifa ya Ireland Kaskazini au Jamhuri ya Ireland.
Uswis yenyewe huenda ikacheza na mshindi wa pili kutoka kundi C, ambao kwa sasa ni Poland lakini Ujerumani au Ireland Kaskazini pia huenda wakawa wapinzani wao.
Katika mchezo mwingine, timu ya taifa ya Albania imerekodi ushindi wake wa kwanza kwenye michuani ya mwaka huu, baada ya kuifunga timu ya taifa ya Romania, ushindi ambao sasa umefufua matumaini ya timu hiyo kutinga hatua ya 16 bora.
Kikosi cha kocha Giovanni de Biasi kinamaliza kwenye nafasi ya tatu kwenye kundi A kwakuwa na alama tatu, na sasa inasubiri kujua ikiwa itakuwa miongoni mwa timu bora zilizomaliza kwenye nafasi ya tatu.
Mchezaji anayekipiga na klabu ya FC Zurich, Armando Sadiku ndiye aliyekuwa muuaji wa bao la ushindi kwa timu yake, baada ya kufunga kwa kichwa akitumia vema mpira wa pasi uliopigwa na Ciprian Tatarusanu.
Ikiwa timu ya taifa ya Albania itafanikiwa kuingia kwenye hatua ya 16 bora, basi huenda ikacheza na mshindi wa pili kutoka kwenye kundi B, ambalo sasa lina timu za Uingereza na Wales lakini pia timuj kutoka kundi C ambalo linahusisha timu ya Ireland Kaskazini.