Timu ya taifa Italia yarudia historia ya mwaka 2000
Mechi za kundi E ziliendelea Jumatatu ya wiki hii ambapo miamba minne ilishuka dimbani kuanza harakati za kutafuta kucheza hatuja ya fainali huku timu ya taifa ya Italia ikiiadhibu Ubelgiji.
Imechapishwa:
Mchezo wa awali wa kundi E ulizikutanisha timu ya taifa ya Jamhuri ya Ireland iliyokuwa ikicheza na Sweden, kwenye mchezo ambao ulishuhudia timu hizi zikimaliza dakika tisini zikitoshana nguvu ya bao 1-1.
Mchezo ambao ulikuwa ni wakukata na shoka na uliokuwa unasubiriwa kwa hamu kubwa, ni ule uliozikutanisha timu ya taifa ya Ubelgiji iliyokuwa na kibarua dhidi ya Italia kwenye mchezo uliokuwa wa kuvutia kwa dakika zote 90.
Mlinda mlango wa timu ya taifa ya Italia, mkongwe Gianluigi Buffon ndiye aliyekuwa kinara kwa timu yake, ambapo aliokoa michomo kadhaa iliyoelekezwa langoni kwake na washambuliaji wa Ubelgiji wakiongozwa na Romelu Lukaku na Origi.
Kwenye mchezo huu timu ya taifa ya Italia ilifanikiwa kuchomoza na ushindi wa mabao 2-0, na kurejelea historia ambayo iliwahi kushuhudiwa wakati timu hizi zilipokutana kwenye hatua ya makundi michuano ya mwaka 2000.
Magoli ya Italia yalifungwa na wachezaji, Emanuele Giaccherini kwenye dakika ya 32 ya mchezo na lile la mwishoni likifungwa kwenye muda wa nyongeza baada ya dakika tisini likifungwa na Graziano Pelle aliyeunganisha mpira wa pasi kutoka upande wa kulia.