Pata taarifa kuu
EURO 2016

Sheria mpya za soka kujaribiwa kombe la Ulaya 2016

Sheria mpya za mchezo ambazo ziliamuliwa na bodi ya shirikisho la kimataifa la mpira wa miguu, na ambazo zimeanza kufanya kazi kuanzia Juni mosi mwaka huu, kwa mara ya kwanza zitashuhudiwa zikitumika kwenye michuano ya kombe la Ulaya inayoanza kutimua vumbi nchini Ufaransa. 

Waamuzi wa shirikisho la soka barani ulaya Uefa, Mark Cluternberg
Waamuzi wa shirikisho la soka barani ulaya Uefa, Mark Cluternberg Reuters / Kai Pfaffenbach Livepic
Matangazo ya kibiashara

Sheria hizi zilipitiwa upya kwa lengo la kuboresha muundo na namna ambavyo baadhi ya vifungu vya maneno kwenye sheria hizi vinapaswa kutumika, mabadiliko haya pia yanahusu sheria halisi zilizobadilishwa kwa kufuata misingi ya ufahamu.

Mabadiliko hayo yanahusu: Sheria ya kuanzisha mpira, ambapo sasa mpira unaweza kuhamishwa kuelekea upande wowote kinyume na ilivyokuwa hapo awali ambapo wakati mechi inapoanza ilikuwa ni lazima mpira uelekee mbele.

Sheria nyingine iliyoboreshwa ni pamoja na inayohusu mchezaji aliyeumia uwanjani na mchezaji aliyemchezea madhambi kuonywa kwa kadi ya njano au nyekundu, sasa ataruhusiwa kupatiwa matibu ndani ya uwanja kwa dakika na kisha kuendelea na mchezo, ambapo awali ilikuwa anatolewa nje ya uwanja kupatiwa matibabu, sheria hii ya awali ilikuwa inaipa timu pinzani upendeleo wa kumiliki mchezo kwakuwa upande mwingine umepungukiwa mchezaji.

Mshambuliaji wa Real Madrid, Christian Ronaldo aki[atiwa matibabu uwanjani, kwa sheria mpya za uefa mchezaji atatibiwa akiwa ndani ya uwanja
Mshambuliaji wa Real Madrid, Christian Ronaldo aki[atiwa matibabu uwanjani, kwa sheria mpya za uefa mchezaji atatibiwa akiwa ndani ya uwanja Reuters / Kai Pfaffenbach Livepic

Mjumbe wa kamati ya waamuzi ya UEFA na kiongozi wa kamati ndogo ya ufundi inayohusika na kuandika upya sheria za mchezo, David Elleray, ameeleza kufurahishwa na maboresho yaliyofanyika na kwamba zitafanyiwa majaribio wakati wa michuano ya kombe la Ulaya mwaka huu.

Elleray, mwamuzi wa zamani kwenye ligi kuu ya Uingereza, amesema “kwa mtazamo wa kidunia, hii ni nafasi ya kipekee kuionesha dunia mabadiliko haya ni nini, yatusaidie kuwaelimisha waamuzi duniani kote, na kwanjia hiyo UEFA inafanya kazi nzuri kuisaidia dunia kuelewa mabadiliko ya sheria hizi.” alisema.

Mjumbe huyo ameongeza kuwa mabadiliko haya ya sheria za mchezo yataisaidia UEFA na mashindano ya mwaka huu ya kombe la Ulaya yatakuwa bora zaidi kutokana na kilichofanyika.

Michuano ya Ulaya ya mwaka huu, pia itashuhudiwa kuanza kutumika kwa majaribio ya miaka miwili, sheria ya kutoa adhabu, ambayo awali ilihusu kutolewa nje, kupewa penati na kufungiwa ikiwa utamzuia kwa makusudi mchezaji aliyekuwa na nafasi nzuri ya kufunga goli kwenye eneo la hatari.

Mwamuzi Mark Cluternberg akimuonesha kadi ya njano mchezaji wa Atletico Madrid wakati wa mchezo wa fainali na Real Madrid
Mwamuzi Mark Cluternberg akimuonesha kadi ya njano mchezaji wa Atletico Madrid wakati wa mchezo wa fainali na Real Madrid Reuters / Kai Pfaffenbach Livepic

Kwenye mabadiliko haya mapya, waamuzi watatoa kadi ya njano na sio kadi nyekundu, lakini ikiwa tu mlinda mlango au beki alikuwa akijaribu kwa dhati na kwa nia njema kuuchukua mpira kutoka kwa mchezaji wa timu nyingine na kumchezea madhambi.

Mkuu wa kamati ya waamuzi ya Fifa, Pierluigi Collina amesema kuwa “UEFA kwa miaka kadhaa sasa imekuwa ikijaribu kufanyia marekebisho sheria ya mchezo na ninayofuraha kuona majaribi yataanza kutekelezwa wakati wa michuano ya kombe la Ulaya. Mabadiliko haya yanarejesha haki kwa adhabu ya penati, kadi nyekundu na kutolewa nje ambayo ilikuwa kali sana ikiwa mchezaji alijaribu kwa nia njema kuuchukua mpira.

Michuano ya mwaka huu pia ya kombe la Ulaya itashuhudia kwa mara ya kwanza UEFA ikitumia teknolojia ya mstari wa goli. Pierluigi Collina anasema kuwa teknolojia ya mstari wa goli na nyingeza ya mwamuzi msaidizi itasaidia kufanya mchezo uwe mzuri na wa haki.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.