Senegal na Burkina Faso kumenyana leo Ijumaa
Fainali ya mchezo wa soka katika mashindano ya michezo ya Afrika inayoendelea jijini Brazavile nchini Congo inachezwa leo Ijumaa kati ya Senegal na Burkina Faso.
Imechapishwa:
Vijana wa Burkina Faso walifuzu baada ya kuifunga Nigeria kwa mabao 3 kwa 1 katika nusu fainali ya kusisimua siku ya Jumanne jioni, huku Senegal nayo ikifuzu kwa kuwashinda wenyeji Congo Brazaville pia kwa mabao 3 kwa 1.
Kumbuka kuwa mashindano haya yaliwashirikisha wachezaji wasiozidi umri wa miaka 23.
Alhamisi wiki hii, Nigeria walimaliza katika nafasi ya tatu baada ya kuwafunga wenyeji Congo kwa mabao 5 kwa 3 baada ya mchuano huo kumalizika kwa sare ya kutofunga.
Kabla ya fainali hiyo kutakuwa na fainali ya wanawake kati ya Ghana na Cameroon.
Michuani hiyo itachezwa katika uwanja wa soka wa Kintele.
Mbali na soka pia kutakuwa na fainali ya mchezo wa kikapu kwa upande wa wanaume na wanawake.
Kwa upande wa wanawake Nigeria itacheza na Mali, huku Angola ikipambana na Misri kwa upande wa wanaume.
Nusu fainali ya mchezo wa Mkono au Handball pia inachezwa leo Ijumaa, kwa upande wa wanawake, Senegal watachuana na Cameroon, Angola na Nigeria.
Upande wa wanaume wenyeji Congo watachuana na Misri huku Nigeria wakipambana na Angola.
Michezo hii itamalizika Jumamosi wiki hii.